SAKATA la mkataba wa Kampuni ya Lugumi Enterprises
limechukua suara mpya, baada ya Kambi ya Upinzani kusema kuwa itahakikisha
mbivu na mbichi za mkataba huo, zinajulikana katika mkutano wa Bunge la Bajeti
unoanza kesho mjini Dodoma.
Kampuni hiyo iliingia mkataba na Jeshi la Polisi
mwaka 2011 na kupewa zabuni ya Sh bilioni 37, kwa ajili ya kufunga mashine za
alama za vidole katika vituo vya polisi, huku ikidaiwa kushindwa kutekeleza
mkataba huo na hivyo kuisababishia Serikali hasara ya mabilioni ya fedha.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Waziri Kivuli wa
Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbless Lema alisema Watanzania watajua ukweli kuhusu
utapeli uliofanywa na kampuni hiyo dhidi ya Jeshi la Polisi.
Lema ambaye pia ni Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema),
alisema kambi ya upinzani itahakikisha umma unapata ukweli juu ya sakata hilo,
ambalo linaonekana kujumwisha baadhi ya vigogo wa Serikali.
Lema alisema nyaraka zinaonyesha kuwa mkataba huo
ulisainiwa mwaka 2011 kati ya Kampuni ya Lugumi na Jeshi la Polisi, ulikuwa ni
kwa ajili ya kufunga mashine za utambuzi wa vidole katika vituo 108, kwa
gharama ya Sh bilioni 37.
“Wakati mkataba wa kazi unasema hivyo, kampuni hiyo
imefunga mashine katika vituo vya polisi 14 tu, huku kampuni hiyo ikilipwa Sh
bilioni 34 za walipa kodi.
“Nikiwa msemaji wa wizara hii kupitia kambi ya
upinzani, suala la Lugumi nitalishughulikia vizuri pale bungeni,
hachomoki…vijana wa sasa wanasema nitakula naye sahani moja.
“Kampuni hii inaonekana wazi imesheheni watoto wa
vigogo na makamishina wa Jeshi la Polisi, sitaki kukurupuka lakini ukweli wote
ninao jambo hili halitazimika hata kidogo,” alisema Lema.
Alisema wakati wote wa mjadala juu ya sakata hilo
amekuwa kimya na kusema kwamba ukimya wake unakishindo, kwani amelifuatilia kwa
undani sakata hilo tangu lilipoanza.
“Suala hili ni zito limesemwa sana hadi kufikia
hatua ya kupelekewa kwenye kamati za Bunge, lakini bado limeshindwa kujadiliwa,”
alisema.
Alisema Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC),
ina mamlaka kamili ya kufanya mambo yote, bila kushurutishwa, lakini anashangaa
kuona katika suala hilo kamati hiyo imekosa makali.
“Kamati hii imepewa mamlaka kamili ya kusimamia na
kushughulikia masuala yote yanayohusu fedha za Serikali na hapa kuna ufisadi wa
mabilioni ya fedha, …inawezekana vipi iitishe mkataba halafu iporwe na kamati
nyingine?
“Sitaki kueleweka vibaya, makamu mwenyekiti wa ile
kamati hana uwezo, siku zote kamati inapaswa kuongozwa na mpinzani…kwa mtindo
huu unategemea nini?
“Inatakiwa mwenyekiti ambaye anaweza kuchambua na
kuelewa mambo kwa mapana zaidi, anatakiwa mtu nyeti badala yake walipanga
kamati wanavyotaka wenyewe.
“Hapa ndiyo maana nahoji uadilifu wa Rais John
Magufuli uko wapi katika suala zito kama hili…amejipambanua ni kiongozi wa
kupambana na ufisadi, rushwa nilitegemea angekuwa wa kwanza kuhoji au kutoa
tamko juu ya sakata hili.
“Unajua hata Mungu ameumba ndege wengi, wapo wenye
mabawa marefu, mafupi, wanaokula sana na wengine kidogo…maana yake ni kwamba
kuna maeneo lazima yashikwe na wapinzani,” alisema Lema.
Alisema kutokana na mwenendo wa suala hilo, ni wazi
kamati za Bunge zimeanza kutoa nafasi kubwa ya kuchezewa tofauti na miaka ya
nyuma.
“Huu ni mwanzo wa kuchezea kamati za Bunge, siku
zote mambo haya hupikwa huko kabla ya kupelekwa pale bungeni…nasema tumejipanga
katika hili,”alisema Lema.
Huku akionekana kukerwa na usiri wa mkataba huo,
Lema alisema suala hilo ni kubwa mno kwa sababu inaonekana linagusa maslahi ya
wengi.
“Namwomba sana Rais Magufuli asiendelee kukaa kimya,
najua ana ujasiri mkubwa au kuna baadhi ya mambo anayoogopa? nadhani anapaswa
kutoa mwelekeo.
“Kampuni ya Lugumi ina vigogo, yeye ni nani,
tutabana maisha yake ya mbwembwe na sifa nyingi mjini hachomoki tutakula naye
sahani moja,” alisema Lema.
Sakata lilivyoanza
Aprili 6, mwaka huu Kamati ya Bunge ya Hesabu za
Serikali (PAC) chini ya Makamu Mwenyekiti wake, Aeshi Hilaly walibaini utata
mkubwa wa utekelezaji wa mkataba huo na kuagizwa upelekwe mbele ya kamati hiyo
ili wajumbe waweze kujadili.
PAC iligundua madudu hayo, wakati watendaji wa Jeshi
la Polisi walipokuwa wakihojiwa na kamati hiyo juu ya utendaji wa shughuli zao.
Baada ya hapo, kumekuwa na taarifa nyingi zakiwamo
za kutoka Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano ya Bunge ya Bunge kuwa
kilichombwa na PAC ni taarifa ya utekelezaji wa mkataba huo na si mkataba
wenyewe.
CUF.
Kwa upande wake Chama cha Wananchi (CUF), kimewataka
wabunge kuhakikisha wanaipitia kwa umakini Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani
ya Nchi na endapo hakutakuwa na maelezo ya kina kuhusu kashfa ya ufisadi wa
Kampuni ya Lugumi waipinge.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Naibu
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa chama
hicho (Bara), Abdul Kambaya alisema haiwezekani mabilioni ya Watanzania yakapotea
bila maelezo ya kina.
Alisema Serikali inapaswa kueleza matumizi ya Sh
bilioni 37 ambazo zilitakiwa zitumike kwa ajili ya kufunga mashine za utambuzi
wa alama za vidole katika vituo vya polisi zaidi ya 100 nchini kote, lakini
hadi sasa ni vituo 14 tu vilivyofungwa na havijulikani vilipo vituo hivyo.
Kambaya alisema katika sakata hilo kuna harufu ya
ufisadi lakini hadi sasa hakuna maelezo ya kina yanayotolewa kuhusu Kampuni ya
Lugumi iliyopewa zabuni hiyo.
“Wabunge mnahaki ya kupinga bajeti hiyo kama
hamtapata maelezo ya kina kuhusu kampuni hiyo na matumizi ya fedha hizo, naomba
mchukue hatua kwa kuwa fedha hizo ni zetu na zingeweza kusaidia sekta
nyingine,”alisema Kambaya.
Aliongeza kuwa, wabunge waangalie kwa makini na
kuzipa kipaumbele bajeti ambazo zimetoa kipaumbele kwenye sekta ya elimu, afya
na miundombinu.
Kambaya alisema Watanzania wanahitaji kubadili mfumo
wa uongozi hapa nchini ili kila mmoja aweze kutoa mawazo yake na uamuzi uwe wa
ushirikishwaji baina ya watu wote.
Pia alisema alimwomba Rais Dk.John Magufuli
kuingilia kati na kuchukua uamuzi stahiki kuhusu sakata la umeya wa Jiji la Tanga
ambalo bado linatia shaka.
“Ni vema wabunge suala la umeya wa Jiji la Tanga
mlizungumze kwa umakini pindi mtakapoanza vikao vya Bunge ili tupate majibu ya
kueleweka kama ilivyotokea hapa Dar es Salaam,”alisema Kambaya.
Kwa upande wake, mchambuzi wa mambo ya siasa Julius
Mtatiro alisema anaishangaa serikali kutenga bajeti ya Wizara ya Viwanda na
Biashara ya Sh bilioni 100 kwa mwaka 2016/2017 wakati ujenzi wa kiwanda cha Dangote kilichopo mkoani Mtwara kimetumia
Sh bilioni 1000, hivyo itatumia muda wa miaka 10 kwa Tanzania kujenga kiwanda
kimoja.
Alisema nchi haina viwanda na hakuna jitihada
zinazofanyika hivyo majipu yataendelea kutumbuliwa lakini matatizo yatazidi
kuongezeka.
“Bila kuongeza jitihada kwenye sekta ya viwanda
vijana wengi wataishia mitaani kwakuwa Serikali ina uwezo wa kuajiri kila mwaka
watu 50 kitakachofanyika maeneo mengi yatakuwa hayana huduma muhimu,”alisema
Mtatiro.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia
(CUF) alisema Serikali lazima ijipange kuwasaidia waathirika wa mabondeni kwa
kuwalipa fidia.
Alisema wananchi wa Kinondoni wa Mto Ng’ombe
waliowekewa alama ya X nyumba zao haziwezi kubomolewa hadi watakapolipwa fidia.
“Tumejipanga kama nyumba zitabomolewa ni lazima
wananchi walipwe fidia zao na kwa wale waliovunjiwa bila fidia tutafungua kesi
mahakamani,”alisema Mtulia.
Naye Mbunge wa Temeke, Abdallah Mtolea (CUF) alisema
Magufuli anatumbua vipele wao wataenda kutumbua majipu bungeni.
Wakati huohuo, Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Bonifas
Jacob alisema kuanzia sasa wananchi wa Kinondoni watanufaika na huduma za bure kwa
kupata huduma za afya bure.
Alisema wananchi hao watalipa Sh 40,000 kwa mwaka
ambapo wataenda katika hospitali za serikali pamoja na zahanati kupata huduma
za afya.
Jacob alisema wazee 34,000 watanufaika na huduma za
afya bure ambapo watatambuliwa kila mtaa na kupewa kadi maalum za matibabu.
Kwa upande wa wajumbe wa mtaa sasa watalipwa Sh
30,000 kila mwezi badala ya Sh 5,000 na
wenyeviti wa serikali za mitaa watapewa Sh 100,000 kwa mwezi badala ya Sh
50,000 waliyokuwa wakilipwa awali.


0 comments:
Post a Comment