Rais
John Magufuli jana alikutana ana kwa ana na rafiki yake, Charles
Kitwanga ikiwa ni siku 80 baada ya kumvua cheo cha Waziri wa Mambo ya
Ndani kwa kosa la kuingia bungeni kujibu maswali akiwa amelewa.
Wawili hao walikutana kwenye Jimbo la Misungwi ambako Rais alisimama akitokea Wilaya ya Sengerema ambako alihutubia wananchi.
Rais
alitengua uteuzi wa Kitwanga Mei 20, wakati sakata la utekelezwaji
mbovu wa mkataba wa Sh37 bilioni baina ya Jeshi la Polisi na kampuni ya
Lugumi Enterprises likivuma kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano.
Lakini
jana, hali ilionekana ya kikazi zaidi wakati Rais alipofika kwenye
jimbo hilo. Kitwanga, ambaye ni mbunge wa Misungwi mkoani Mwanza,
alitumia nafasi hiyo kukutana na Rais kwa mara ya kwanza hadharani,
kuwasilisha kero za wananchi wake, hasa ya maji.
Katika tukio hilo
lililovutia hisia za waliokuwepo, Rais aliuthibitishia umma kuwa yeye na
Kitwanga ni marafiki wa muda mrefu, alipokuwa akijibu ombi la mbunge
huyo la kutaka Serikali itatue kero ya maji eneo la Usagara na Misungwi.
“Kitwanga ni rafiki yangu. Tayari Serikali imepanga kutumia zaidi
ya Sh8 bilioni kutekeleza mradi mkubwa wa maji maeneo ya jimbo la
Misungwi, ikiwemo Usagara,” alisema Rais Magufuli akiwa amesimama kwenye
gari lililofunuliwa upande wa juu.
Katika sakata la Lugumi, wabunge
walitaka suala lijadiliwe baada ya taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu
wa Hesabu za Serikali (CAG) kubaini kuwa kampuni hiyo ilishindwa kufunga
mashine za kielektroniki za kuchukulia alama vidole kwa mujibu wa
mkataba.
Mkataba huo ulisainiwa mwaka 2011 lakini hadi CAG alipokuwa
akifanya ukaguzi mwaka jana, ni vituo 14 tu kati ya 118 vilivyokuwa
vimefungwa mashine hizo, huku Lugumi Enterprises ikiwa imelipwa Sh36
bilioni ambazo ni zaidi ya asilimia 90 ya fedha za mkataba huo.
Kitwanga
alihusishwa na sakata hilo kutokana na dhamana yake na pia kuwa na hisa
kwenye kampuni ya Infosys, ambayo ni wakala wa kampuni ya Dell
inayozalisha kompyuta, kuhusishwa kutoa vifaa hivyo.
Hata hivyo,
Juni 22, Kitwanga aliwaambia waandishi wa habari nyumbani kwake kuwa
Infosys haina uhusiano wowote wa kibiashara na Lugumi.
Jitihada za
wabunge, hasa wa upinzani kutaka kuzungumzia suala hilo zilikwama kwa
maelezo ya kutaka kusubiri ripoti ya kamati ndogo iliyoundwa kuchunguza
suala hilo.
Ripoti hiyo iliwasilishwa mwishoni mwa vikao vya Bunge
la Bajeti na haikujadiliwa baada ya Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kusoma
maagizo ya Bunge kwa pande zinazohusika kwenye mkataba.
Kabla ya
suala hilo kuzuiwa kujadiliwa, wabunge walikuwa wakidai kuwa Rais na
Kitwanga ni marafiki wa karibu na baadaye mitandao ya kijamii ikasambaza
mkanda unaoonyesha jinsi walivyokuwa wakijadili suala la Magufuli
kuchukua fomu ya kugombea urais.
Kwenye kampeni za Uchaguzi Mkuu wa
mwaka jana, Magufuli alimnadi Kitwanga kwa kueleza kuwa anamfahamu kwa
kuwa walisoma wote na ni rafiki yake.
Kabla ya kwenda Sengerema kwa
kivuko jana, Rais alihutubia wilayani Sengerema ambako aliendelea na
onyo lake dhidi ya watu anaosema wanataka kuvuruga amani.
Akihutubia
mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Mnadani mjini
Sengerema, Rais Magufuli aliwataka wenye lengo la kuvuruga amani
kumsubiri amalize kipindi chake cha uongozi kwa sababu hatawapa fursa
hiyo.
“Wapo wanaotumia taasisi za kisiasa na kidini kujaribu
kuvuruga amani ya nchi. Hawa hatutawapa fursa hata kidogo kwa sababu
amani ya nchi ikivurugika hakuna hata mmoja atakayebaki salama; sote
tutaangamia,” alisema Rais Magufuli
Aliwakumbusha wakazi wa
Sengerema jinsi walivyowapokea wakimbizi kutoka nchi jirani ya Rwanda
miaka ya tisini wakati taifa hilo lilipoingia kwenye mauaji ya kimbari
yaliyoishia kwa watu zaidi ya milioni moja kupoteza maisha.
“Tunayo
mifano hai ya mataifa yaliyochezea amani na kusambaratika. Rwanda
ilipitia njia hiyo kabla ya kusimama upya.Zipo Libya na Somalia ambazo
hadi sasa zimegawanyika vipande vipande,” alisema Rais Magufuli.
Aliwataka
Watanzania kulinda kwa udi na uvumba amani na utulivu ulioasisiwa na
Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wengine, kwa kuwapiga
vita wanaovuruga amani hata kama ni ndugu, jamaa, marafiki, wanachama au
waumini wenzao.
Rais anaendelea kutoa onyo hilo wakati Chadema
ikiendelea kusisitiza maazimio ya Kamati Kuu ya chama hicho ya kuitisha
mikutano ya hadhara nchi nzima kuanzia Septemba Mosi, ikiwa ni sehemu ya
kampeni itakayoendeshwa na Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (Ukuta),
ambayo tayari baadhi ya wakuu wa mikoa wamepiga marufuku.
Chadema
inadai kuwa uamuzi wa Rais kupiga marufuku mikutano ya kisiasa na
kudhibiti wanasiasa kuhudhuria mikutano hiyo nje ya maeneo yao, ni
kukiuka Katiba, Sheria ya Vyama vya Siasa, Kanuni za Maadili za Vyama
vya Siasa na haki za binadamu.
Kuhusu vita dhidi ya ufisadi, Rais pia
aliahidi kuongeza kasi kupitia mtindo wake wa kutumbua majipu, huku
akilishukuru Bunge kwa kupitisha sheria itakayosaidia vita hivyo pamoja
na kupitisha bajeti ya Sh2 bilioni ya kuanzisha Mahakama Maalumu ya
Rushwa.
Akizungumzia suala la chakula nchini, Rais John Magufuli
amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya kuhakikisha maeneo yao yanazalisha
chakula cha kutosha, akionya kuwa Serikali haitatoa chakula cha msaada
kwa watakaokumbwa na njaa kutokana na uzembe na uvivu.
Rais alisema
kazi ya kulisha familia ni jukumu la wakuu wa familia na kuongeza kuwa
kila familia ina wajibu kulima na kuhifadhi chakula cha kutosha mahitaji
ya kipindi chote cha mwaka.
“Kazi ya Serikali ni kutoa huduma kama
barabara, dawa na mahitaji mengine ya kijamii, lakini si msaada wa
chakula kwa watu wavivu,” alisema Rais Magufuli.
Kuhusu usafiri wa
Reli ya Kati, Rais alisema tayari Serikali imetengeneza zaidi ya Sh1
trilioni kwa ajili ya mradi wa kubadili reli hiyo kuwa katika viwango
vya kimataifa.
Alisema serikali pia inakusudia kununua meli mpya ya
abiria itakayokuwa ikifanya safari Ziwa Victoria yenye uwezo wa kubeba
abiria 1,000 na tani 800 ya mizigo.
Pia alisema Serikali imeweka
mikakati ya kukabiliana na uvuvi haramu kwenye Ziwa Victoria, ambalo
lilikuwa likitoa fursa za ajira kwa watu zaidi ya milioni 6 katika
nyanja mbalimbali, fursa ambazo alisema zimepungua maradufu kutokana
vitendo vya uvuvi haramu.
Rais Magufuli, ambaye atatumia ziara yake
kukagua miradi ya maendeleo ikiwamo ujenzi wa daraja la juu la waenda
kwa miguu eneo la Furahisha pamoja na upanuzi wa barabara ya
Ghana-Pasiansi kutoka njia mbili za sasa hadi nne, leo anatahutubia
mkutano wa hadhara kwenye viwanja vya Furahisha, Kirumba jijini Mwanza.
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)

0 comments:
Post a Comment