Image
Image

SERIKALI YATANGAZA OPERESHENI KUWATIMUA WAHAMIAJI HARAMU NCHINI.


Dk. Emmanuel Nchimbi Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchini.

Serikali imetangaza rasmi kuendesha operesheni kabambe, itakayofanyika kwa kushtukiza wakati wowote kuanzia sasa, kuwaondoa kwa nguvu nchini wahamiaji haramu waliokaidi agizo la Rais Jakaya Kikwete, lililowataka kurejea makwao kwa hiari yao ndani ya wiki mbili, kuanzia Julai 29, mwaka huu.



Wahamiaji hao haramu, ambao wamekuwa wakiishi nchini kinyume cha sheria za nchi na taratibu za Idara ya Uhamiaji, wanatoka katika nchi za Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).



Agizo hilo lilitolewa na Rais Kikwete Julai 29, mwaka huu, alipofanya ziara katika Mkoa wa Kagera, ambako aliwapa wiki mbili wahamiaji haramu wawe wamerudi makwao kwa hiari yao, vinginevyo wangekamatwa katika operesheni maalumu ya kijeshi baada ya muda huo kuisha.



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, aliwaambia waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana kuwa operesheni hiyo aliyoiita ya “ghafla”, itafanyika baada ya Rais Kikwete kumpa kibali cha kuiendesha.



Alisema maeneo yatakayohusika zaidi na operesheni hiyo ni ya mikoa ya Kanda ya Ziwa na kwamba, hawatakuwa na ‘msalie mtume’ kwa mgeni yeyote atakayebainika kuishi nchini isivyo halali. 
 

 
“Nimeelekezwa na Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, muda wa kuwaondoa nitakapoona inafaa.

 

Vyombo vya dola vitaniambia ni lini. Katika muda huu hatutafanya mzaha na jambo hili.

 Hatutavumilia tena wageni haramu,” alisema Nchimbi.



Aliwataka viongozi wa serikali za vijiji vilivyoko katika mikoa ya kanda hiyo kufahamu kwamba, ni kosa kisheria kushirikiana na wahamiaji haramu.



Kutokana na hilo, alionya kuwa watakaobainika wakiwaficha wahamiaji haramu, watakamatwa na kufikishwa mahakamani.



Awali, Waziri Nchimbi alisema baada ya agizo hilo la Rais Kikwete, mwitikio umekuwa mzuri na kwamba, hadi kufikia usiku wa Agosti 18, mwaka huu, wahamiaji haramu 10,672 walikuwa wameondoka nchini na mali zao.



Alisema kati ya wahamiaji hao haramu, katika Mkoa wa Kagera, Wanyarwanda walikuwa 6,088, Warundi 4,000 na Waganda 269.

Kwa mujibu wa Waziri Nchimbi, katika Mkoa wa Kigoma, walioondoka ni 150, kati yao Warundi ni 142 na DRC ni wanane.

Alisema katika Mkoa wa Geita wahamiaji haramu walioondoka ni 165; kati yao Wanyarwanda ni 126 na Warundi 39.

Hata hivyo, alisema kazi ya wahamiaji hao kuondoka nchini, bado inaendelea na kuwataka wananchi hususan wa Mkoa wa Kagera kuwaacha waondoke bila kunyanyaswa, ikiwamo kupora mali zao.

Hata hivyo, alisema kati ya wahamiaji haramu walioondoka, 14 wamerudi tena nchini na kukiita kitendo hicho kuwa ni cha “kichokozi.

” 

Alisema Rais Kikwete alitoa agizo lile baada ya wizara kufanya utafiti na kumpa taarifa na kwamba, wahamiaji haramu wanaosumbua ni wale wanaomiliki vyeti bandia vya kuzaliwa.

NIPASHE
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment