Image
Image

CHIKAWE AMWOMBA JK ASAINI MUSWAADA KUEPUSHA VURUGU.


Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema mikutano wanayoifanya na asasi za kiraia imebainisha kwamba uteuzi wa Tume ya Katiba ulifanyika kwa ubaguzi.

Dar es Salaam/Simiyu. 

Wakati vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi vikiendelea na shinikizo la kutaka Rais Jakaya Kikwete asitie saini Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe amemwomba mkuu huyo wa nchi auridhie ili kuepusha vurugu ambazo zinaweza kujitokeza katika kikao kijacho cha Bunge.
Ameonya kuwa muswada huo ukirudi bungeni unaweza kusababisha vurugu kubwa zaidi ya zile za mara ya kwanza kutokana na tofauti kati ya wabunge wa CCM na wale wa vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Chikawe alisema kelele zinazopigwa na wapinzani hivi sasa hazisaidii kwa kuwa muswada huo ulipitishwa baada ya taratibu zote kukamilika.

Alisema kuwa kutokana na hali hiyo, atamshangaa Rais Kikwete ikiwa atasikiliza kelele za wapinzani kwa sababu walishirikishwa kupitia kamati na hata bungeni kabla ya kupitishwa kwake.

“Nitamshangaa sana Rais Kikwete kama atashindwa kusaini muswada huo kwa sababu ya kelele za wapinzani. Tuliwashirikisha katika kila mchakato kabla na baada ya kuuwasilisha bungeni,” alisema Chikawe.

Alisema kitendo cha wapinzani hao kujiunga pamoja na kuanzisha kampeni za kuwahamasisha wananchi ili waukatae muswada hakisaidii lolote, kwa sababu sheria zote zinatungwa bungeni na siyo kwenye Viwanja vya Jangwani wala Ikulu.

Vyama vyampinga JK

Wakati Chikawe akisema hayo, viongozi wa Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi wameshikilia msimamo wao kwamba wataendelea kupinga muswada huo uliopitishwa na Bunge, Septemba 6, mwaka huu.

Wakizungumza Dar es Salaam jana walipokutana na Shura ya Maimamu ikiwa ni mwendelezo wao wa kukutana na asasi za kiraia, viongozi wakuu wa vyama hivyo, walisema kamwe kasi yao ya kutaka kutosainiwa kwa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba haiwezi kupunguzwa kwa namna yoyote kwa kuwa wanatetea masilahi ya Watanzania na siyo mtu binafsi.

Kauli yao imekuja siku moja baada ya Rais Kikwete kusema kuwa baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakisema uongo kuhusu mchakato wa Katiba unavyokwenda.

Wanasiasa pia hao wamepinga matumizi ya kauli za kibabe kwenye mchakato huo na kuonya kuwa nguvu ya dola haiwezi kushindana na nguvu ya umma.
Mbali na hayo, wanasiasa hao walisisitiza kwamba hawatapiga magoti kuomba Katiba Mpya, kwani ni ya Watanzania wote na si mali ya wanasiasa, chama cha siasa wala wabunge.

Rais Kikwete alikaririwa na magazeti mbalimbali jana akipinga madai ya wapinzani kuwa hakuzingatia maoni yao wakati wa uteuzi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

“Nafahamu kwamba tunaambiwa tunasema uongo, lakini ni vizuri ifahamike wazi kuwa hatuwezi kupunguzwa nguvu na kauli hizo alizozitoa Rais Kikwete, kwani msimamo tulionao ni kuendelea kutetea Watanzania,” alisema Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Mbowe alimshauri Rais Kikwete atumie busara kwa kutosaini mkataba huo ili mchakato uende vizuri.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema mikutano wanayoifanya na asasi za kiraia imebainisha kwamba uteuzi wa Tume ya Katiba ulifanyika kwa ubaguzi.

“Tunafahamu kwamba Rais ana nguvu ya kuteua wajumbe wa tume hiyo kwa mujibu wa sheria, lakini kuna taasisi zimekosa wawakilishi kwenye tume, mfano hai ni Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (Shivyawata), walitakiwa wapeleke majina ya watu watatu, lakini hakuna hata mtu mmoja kati yao aliyeteuliwa,” alisema Profesa Lipumba.

Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, James Mbatia alisema viongozi wa Shivyawata waliwaeleza wazi kuwa hawana mwakilishi kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Wanasiasa hao leo wanatarajia kukutana na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (Tec).
Nape alonga

Akizungumzia madai hayo ya upinzani, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema kama wanataka waaminike, watoe ushahidi kuthibitisha wanachokidai.

“Hawa watu ni vigeugeu. Kwanza, Rais alipoteua wajumbe wa Tume, Chadema walijitokeza hadharani na kupongeza. Baadaye haohao waliibuka na kuanza kuishutumu Tume wakisema kuwa imekosa weledi.

“Wakati wa mchakato wa kukusanya maoni, Chadema haohao, ambao waliiona Tume haina weledi, wakapeleka maoni yao hukohuko. Ukifuatilia haya mtu unashindwa kuelewa msimamo wa watu hawa ni upi hasa,” alisema Nape mkoani Simiyu.

SOURCE: MWANANCHI
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment