Ufoo Saro.
DAR ES
SALAAM.
HALI ya mwandishi wa habari wa
Kituo cha Televisheni cha ITV, Ufoo Saro aliyejeruhiwa vibaya baada ya kupigwa
risasi mbili juzi huko Kibamba, Dar es Salaam inazidi kuimarika na jana
alizungumza na gazeti hili na kusema; “Sijambo, naendelea vizuri.”
Ufoo, ambaye amelazwa katika Hospitali
ya Taifa ya Muhimbili, hata hivyo, anazungumza kwa shida kutokana na kukabiliwa
na maumivu baada ya kufanyiwa upasuaji juzi.
Kaka wa marehemu
Anthery Mushi aliyemuua mkwewe, kumjeruhi mzazi mwenzake, Ufoo Saro na kujipiga
risasi, Silva Andrea akizungumza jijini Dar es Salaam jana, kuhusu taratibu za
mazishi ya mdogo wake anayetarajiwa kuzikwa wiki hii, Uru, Moshi Vijijini
mkoani Kilimanjaro. Wa pili kushoto ni kaka mwingine wa marehemu, Isaya
Mushi.Picha na Michael Jamson.
Mwandishi huyo amehamishiwa
katika wodi ya upasuaji wa moyo huku kiongozi wa wodi hiyo, ambaye alikataa
jina lake kuandikwa gazetini, akieleza kuwa walimhamishia huko ili apate muda
zaidi wa kupumzika.
“Watu wanakuja kwa wingi kumjulia
hali, tuliona tumhamishe ili apumzike,” alisema kiongozi huyo.
Kabla ya kupelekwa katika wodi
hiyo, Ufoo alikuwa katika wodi ya Kibasila na baadaye alihamishiwa katika
Chumba cha Wagonjwa Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU).
Ufoo alipigwa risasi na mzazi
mwenzake, Anthery Mushi ambaye alijiua baadaye. Pia Mushi anatuhumiwa kumuua
mama yake Ufoo, Anastazia Saro wakati wa tukio hilo.
Mazishi ya mama yake Ufoo
yamepangwa kufanyika Ijumaa huko Machame mkoani Kilimanjaro.
Ufoo aongea kwa shida
Mara baada ya mwandishi wa gazeti
hili jana kuingia
katika chumba alicholazwa Ufoo
huku akisindikizwa na wauguzi watatu, mwandishi huyo alitoa mkono wake na
kusema; “Njoo hapa unisalimie huku umenishika mkono.”
Huku akionyesha uchovu na kusikia
maumivu, alizungumza kwa tabu na kusema; “Sijambo naendelea vizuri.”
Mara baada ya wauguzi hao kumweleza kuwa kati
ya waandishi zaidi ya 30 waliofika kumjulia hali ni watatu tu ndiyo
walioruhusiwa kumwona alitaka kujua ni kina nani waliobaki nje kwa kuhoji;
“Nani hao wako nje.” MWANANCHI.



0 comments:
Post a Comment