Image
Image

Graca Machel, Waziri Kairuki walia na ndoa za utotoni


Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Angellah Jasmine Kairuki (kushoto) akiongea na Mke wa Rais wa zamani wa Afrika Kusini na mwanaharakai wa haki za wanawake na watoto Bi. Graca Machel (katikati) jijini Dar es Salaam jana (Jumatano, Januari 21, 2014). Kulia ni Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa Linaloshughulikia Idadi ya Watu Duniani (UNFPA) hapa nchini Dkt. Natalia Kanem. Bi. Machel yupo nchini kuunga mkono jitihada za wadau mbalimbali katika kupambana na vitendo vya ukeketaji na ndoa za utotoni.

Na.Mwandishi Wetu 
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Angellah Jasmine Kairuki na Mke wa aliyekuwa rais wa Afrika Kusini, Graca Machel wametoa wito kwa wadau kutoka taasisi za umma na binafsi kuunganisha nguvu ili kuwawezesha watoto wa kike kupata elimu na kuondokana na ndoa za utotoni. 
Bi. Machel, kupitia asasi yake inayojulikana na Mfuko wa Graca Machel (Graca Machel Trust), yupo nchini Tanzania kwa ziara rasmi ya kikazi kuunga mkono jitihada za serikali na taasisi mbalimbali zilizopo nchini kupiga vita ukeketaji na ndoa za utotoni. 
Tangu mwezi Agosti 2014, Mfuko wa Graca Machel kwa kushirikiana na taasisi isiyo ya kiserikali ya ‘Children’s Dignity Forum (CDF)’ na Shirika la Umoja wa Mataifa Linaloshughulikia Idadi ya Watu Duniani (UNFPA), wamekuwa wakianzisha na kuendesha miradi mbalimbali inayolenga kumaliza ndoa za utotoni katika mkoa wa Mara ambao matukio ya ndoa za utotoni yanaelekwa kuwa mengi.
Miradi hiyo ni pamoja na mafunzo kuhusu athari za ndoa za utotoni na ukeketaji kwa maofisa wa Mahakama, Polisi, viongozi wa kidini na kimila pamoja na walimu na wanafunzi.
Akiongea jijini Dar es Salaam jana (Jumatano, Januari 21, 2015), Bi. Machel amesema ingawa serikali na wadau wengine wamefanya jitihada kubwa ili kumaliza ukeketaji na ndoa za utotoni, lakini vitendo hivyo bado vinaendelea na hivyo kuhitajika mkakati unaojumuisha wadau wote ili kuondokana na matatizo hayo yanayotokana na tamaduni potofu.
“Baadhi ya tamaduni zinaweza kubadilishwa, hususan pale zinapodhuru watu, jamii na taifa,” alisema Bi. Machel na kuongeza kuwa nguvu za pamoja zinahitajika kutoka ngazi za chini kabisa.
“Hebu tujaribu kuunda umoja wenye nguvu ili kumaliza ndoa za utotoni. Umoja ambao unajumuisha wadau wa sekta ya umma na binafsi, viongozi wa kimila na kidini, shirikisho la walimu na asasi za kiraia…hili jambo lisiwe la mtu mmoja, liwe letu sote!’ alisema Bi. Machel anayetambulika kama mwanaharakaiti wa kimataifa wa haki za watoto.
Bi.Machel, ambaye taasisi yake inajihusisha na haki za wanawake; haki za watoto; na demokrasia na utawala bora, alisisitiza kuwa umoja huo unapaswa kuwa na mipango mathubuti inayotekelezeka wakati wote hata pale kunapokuwa na mabadiliko ya uongozi wa katika wilaya au vijiji.
Akiongea katika mkutano huo, Naibu Waziri Kairuki alimshukuru Bi. Machel kwa jitihada zake na kumhakikishia kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote wa ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha kuwa watoto wote, hususan wa kike wanapata elimu na ndoa za utotoni na vitendo vya ukeketaji vinamalizika mkoani Mara na nchini kote.


Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Angellah Jasmine Kairuki akisalimiana na Mke wa Rais wa zamani wa Afrika Kusini na mwanaharakai wa haki za wanawake na watoto Bi. Graca Machel jijini Dar es Salaam jana (Jumatano, Januari 21, 2014). Wengine ni wadau kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Maendeleo ya jamii, Jinsia na Watoto, Shirika la Umoja wa Mataifa Linaloshughulikia Idadi ya Watu Duniani (UNFPA) na Asasi isiyo ya kiraia ya Children’s Dignity Forum. Bi. Machel yupo nchini kuunga mkono jitihada za wadau mbalimbali katika kupambana na vitendo vya ukeketaji na ndoa za utotoni.
Naibu Waziri alimweleza Bi. Machel, ambaye aliambatana na Mwakilishi wa UNFPA hapa nchini Dkt. Natalia Kanem na Mkurugenzi Mtendaji waCDF Bw. Koshuma Mtengeti kuwa haki za watoto zimejumuishwa katika Katiba Inayopendekezwa. Aidha, Naibu Waziri Kairuki aliongeza kuwa serikali imeongeza jitihada za kutoa elimu kwa watoto wa kike  na jamii kwa ujumla kuhusu madhara ya ndoa za utotoni na vitendo vya ukeketaji.

Kairuki pia alimweleza Bi. Machel namna katiba mpya inatakavyoisadia serikali katika kusimamia sekta muhimu kama elimu ili kuwawezesha watoto wote, wakiwemo wa kike, kupata haki zao ikiwemo haki ya kupata elimu.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri Kairuki, ili mafanikio makubwa yapatikane, ni muhimu kuwa na mikakati inayojumuisha watunga sera, viongozi wa kidini na jamii zinazojihusisha na vitendo vya ukeketaji na ndoa za utotoni.

Bi. Machel alitarajiwa kuondoka leo (Alhamisi, Januari 22, 2015) kwenda mkoani Mara kukagua utekelezaji wa miradi ambayo inatekelezwa kwa pamoja kati ya serikali, CDF na UNFPA.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment