Image
Image

Rais Kikwete awapa wosia wa amani viongozi wa dini.

RAIS Jakaya Kikwete amewaomba viongozi wa dini nchini kuendeleza hali ya amani na utulivu uliopo nchini kwa kuhakikisha kuwa nchi inabaki na amani, kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, 2015.
Aidha, Rais Kikwete amelishukuru Kanisa Katoliki nchini kwa kuendeleza ushirikiano wake na serikali katika kutoa huduma za kijamii na kusaidia kuleta maendeleo ikiwemo katika sekta ya elimu na afya.
Akizungumza katika sherehe ya kuadhimisha miaka miwili ya Upapa wa Baba Mtakatifu Francis iliyofanyika Juni 26 mwaka huu, nyumbani kwa Balozi wa Vatican nchini Tanzania eneo la Oysterbay Dar es Salaam, alisema amani ya nchi ni lazima iendelee kulindwa.
“Naacha nchi yenye amani na utulivu, nchi ambayo inapitia katika kipindi cha ustawi wa kiuchumi na kijamii ambao haujapata kutokea katika historia ya Tanzania.
“Napenda pia kusisitiza kuwa hakuna binadamu aliyekamilifu. Kwa wale ambao niliwakosea, naomba waelewe ukomo wa uwezo wa binadamu. Hakuna asiyekosea.
Nimejaribu kwa kadri ya uwezo wangu, na nina hakika kuwa mrithi wangu ataendeleza kazi nzuri ambayo nimeifanya katika miaka 10 iliyopita hasa ile ya kujenga na kuimarisha uhusiano kati ya Dola na Kanisa,” alisema Kikwete.
Alisema Dola na Kanisa ni taasisi zinazoendeshwa na binadamu, inatokea wakati mwingine uhusiano kati ya taasisi hizo mbili ukapitia katika mawimbi lakini ni uhusiano unaoendelea kuwepo na kuimarishwa.
Sherehe hizo ziliandaliwa na Balozi Askofu Mkuu Francisco Padilla na kuhudhuriwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Kanisa Katoliki la Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo na maaskofu wengine wa majimbo yote ya Katoliki ya Tanzania.
Katika sherehe hizo, Rais Kikwete pia alitumia nafasi hiyo kuwaaga viongozi wa dini na wakuu wa Kanisa Katoliki akiwasisitizia kuwa anaacha nchi yenye amani na utulivu na nchi inayopitia katika ustawi wa kiuchumi na kijamii ambao haujawahi kutokea katika historia ya Tanzania.
“Kila miaka mitano, Tanzania hupiga kura kupata ridhaa ya wananchi ya kuongoza. Makabidhiano ya madaraka katika Tanzania limekuwa ni suala la amani na tunabakia mfano wenye kung’ara katika Afrika kwa kuruhusu makabidhiano ya amani,” alisema.
Aidha alisema ana imani viongozi wa dini watashirikiana vyema na kiongozi mpya atakayeteuliwa na kuendeleza mema yote aliyoyaacha pamoja na kusimamia vyema mchakato wa uchaguzi na makabidhiano ya uongozi vinakuwa vya amani.
Kuhusu miaka miwili ya uongozi wa Papa Francis, Kikwete alisema kuwa kiongozi huyo ameleta matumaini mapya duniani, ujumbe mpya wa amani, heshima kwa utawala wa sheria, amani na utulivu.
Vilevile ujumbe wake kuhusu changamoto nyingi duniani ikiwemo tabianchi umeongeza sauti yenye nguvu sana kwa namna dunia inavyoendeshwa.”
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment