Image
Image

Kwa hili bila ya kupepesa macho tunaamini Mkapa ameteleza.

Kati ya mambo yaliyozua gumzo kubwa baada ya kumalizika kwa mkutano wa uzinduzi wa kampeni wa Chama cha Mapinduzi (CCM) uliovutia maelfu ya watu kwenye viwanja vya Jangwani jijini Dar es Salaam juzi ni mashambulizi aliyotoa Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho, Benjamin Mkapa, dhidi ya wapinzani.
Bila kutarajiwa, Mkapa ambaye pia ni Rais mstaafu wa awamu ya tatu, alisikika akiwaita wapinzani kuwa ni ‘wapumbavu’ na ‘malofa’. Sababu ya Mkapa kusema yote hayo ilikuwa ni kupinga kile anachodai kuwa ni kitendo cha wapinzani kudai kuwa wanataka kuwakomboa Watanzania wakati kazi hiyo ilishafanywa kitambo na vyama vya kupigania uhuru.
Sisi tunaamini kuwa maneno yaliyotumiwa na Mkapa ni matokeo ya kuteleza kwa ulimi. Hatuamini hata kidogo kuwa aliyatumia kwa usahihi. Hili linatokana na ukweli kuwa wapo watu kadhaa waliokwazika baada ya kusikia kauli hiyo ya Mkapa kwenye mkutano uliokuwa ukifuatiliwa pia na mamilioni ya Watanzania kupitia matangazo ya moja kwa moja ya televisheni.  Hakika, ijapokuwa Mkapa alikuwa akishangiliwa na maelfu ya wanachama wa CCM waliohudhuria mkutano huo, bado ukweli unabaki kuwa kauli yake dhidi ya wapinzani iliwaacha wengi midomo wazi. Kamwe haikutarajiwa kwamba kiongozi huyo mstaafu angefikia hatua ya kutamka maneno hayo yanayochukuliwa na wengi kuwa ni sehemu ya matusi yanayopaswa kuzuiwa na mamlaka zinazosimamia uchaguzi mkuu. 
Kwakweli,‘mpumbavu’ siyo neno zuri kulitamka dhidi ya wengine. Halifai kutumiwa kwa namna aliyoitumia Mzee Mkapa. Miongoni mwa maana zake, kwa mujibu wa Kamusi ya Kiswahili Sanifu, Toleo la Tatu lililotolewa mwaka 2013 na Taasisi ya Ukuzaji Kiswahili (TUKI) na kisha kuchapishwa na Chuo Kikuu cha Oxford, ni pamoja na ‘juha’, ‘fala’ na ‘zuzu’. Yote haya siyo maneno mazuri yanayofaa kutumiwa kwa namna aliyoitumia Mkapa kwani yana muelekeo dhahiri wa kukiuka kanuni inayozuia kauli za kashfa na matusi kwenye mikutano ya kampeni.
Sisi tunapinga matumizi ya maneno ya namna hii kwa sababu kadhaa,mojawapo ikiwa ni ukweli kwamba Mzee Mkapa ni kiigizo cha wengi. Wapo vijana wanaojaribu kumuiga kila afanyalo kwa kuamini kuwa siku moja watatimiza ndoto ya kufikia alipo yeye. Hii maana yake ni kwamba wanaweza pia kuiga maneno hayo wakati wakiwazungumzia watu wanaotofautiana nao kwa hoja, mtazamo na itikadi. Hatari nyingine ni ukweli kuwa kauli hii ya Mkapa yaweza kutoa fursa kwa wanasiasa wengine kufuata mwenendo huo katika kampeni zinazoendelea kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25. Hili linapaswa kuepukwa.
Kadhalika, ikumbukwe kuwa mtu aliye kwenye nyumba ya vioo hapaswi kuanzisha ugomvi wa kurushiana mawe kwani anaweza kujiweka katika hatari ya kupata madhara makubwa  pindi wale anaowashambulia watakapojibu mapigo. Wapinzani wa CCM wasipokuwa na subira wanaweza kujibu mapigo katika kampeni zao kwa kutoa kauli zinazoumiza zaidi ya zile za Mkapa, na hapo watakaoathirika ni wananchi ambao huenda wasipate tena wasaa wa kusikiliza kwa kina sera na ilani za vyama kabla ya kufanya uamuzi siku ya kupiga kura.
Sisi tunaamini kuwa Mzee Mkapa ameteleza. Tunawasihi wanasiasa wengine wawe wavumilivu na kuhakikisha kuwa nao hawatelezi kwa namna iliyoshuhudiwa juzi kwenye viwanja vya Jangwani. Tuzingatie.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment