Image
Image

Maaskofu watatu nchini kuwakilisha ziara ya Papa.

MAASKOFU watatu wa Kanisa Katoliki nchini wanatarajiwa kuiwakilisha Tanzania katika ibada ya misa maalumu, inayotarajiwa kufanyika jijini Kampala nchini Uganda, katika ziara ya kwanza ya Papa Francis barani Afrika iliyopangwa kufanyika kuanzia Novemba 25 hadi 30, mwaka huu.
Ziara hiyo ni ya kwanza Afrika kwa Papa Francis tangu ateuliwe kuwa kiongozi wa takribani Wakatoliki bilioni 1.2 duniani, mwaka 2013. Papa Francis anatarajiwa kutembelea Kenya, Uganda na Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR).
Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Raymond Saba, aliwataja maaskofu hao watakaoiwakilisha Tanzania katika ziara hiyo nchini Uganda kuwa ni Desiderius Rwoma wa Bukoba, Liberatus Sangu wa Shinyanga na Paul Ruzoka wa Tabora.
Akizungumza kwa njia ya simu na gazeti hili, Padri Saba alisema kwa mujibu wa ratiba ya awali iliyotolewa katika mtandao wa Catholic News Service mapema mwezi huu, Papa Francis atawasili nchini Kenya keshokutwa Jumatano, kabla ya kwenda Uganda Ijumaa wiki hii.
“Akiwa Uganda, Papa atatoa heshima kwa ajili ya kumbukumbu ya Waanglikana 23 na mashahidi wa Kikatoliki 22, waliuawa kutokana na imani zao kwa amri ya Mfalme Mwanga II kati ya mwaka 1885 na 1887,” ilieleza taarifa ya mtandao huo.
Novemba 28, mwaka huu atatembelea makaburi ya mashahidi wa Anglikana na Katoliki katika eneo la Namugongo ambako ataongoza ibada kwa ajili ya mashahidi hao jirani na makaburi ya Wakatoliki.
Mjane wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Mama Maria Nyerere amekuwa ni mmoja wa mahujaji wanaotembelea makaburi hayo, Juni 3 ya kila mwaka ambapo Uganda husherehekea Siku ya Mashahidi hao.
Padri Saba alisema ziara hiyo ya Papa Francis ni muhimu hasa katika kipindi hiki kutokana na uhasama unaoendelea Jamhuri ya Afrika ya Kati kati ya waumini wa Kiislamu na Kikristo pamoja na mashambulizi ya kigaidi nchini Kenya.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment