Image
Image

Rais Magufuli nguvu ulioiongeza katika utatuzi wa mgogoro wa kisiasa Zanzibar uendelee.


Rais Dk. John Magufuli, ameongeza nguvu katika jitihada za kusaka suluhu ya mgogoro wa kisiasa wa Zanzibar baada ya kukutana na mgombea urais kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, Ikulu jijini Dar es Salaam, juzi. Mazungumzo baina yao yalifanyika kufuatia ombi la Maalim Seif aliyeomba kukutana na Rais Magufuli.
Hatua hiyo imekuja siku chache baada ya Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) kuiweka Tanzania kiporo wakati wa kikao cha bodi yake kilichofanyika wiki iliyopita jijini Washington, Marekani.
Kikao hicho ndicho kiliahirisha kujadili suala la msaada kwa Tanzania kutokana na mgogoro wa uchaguzi wa Zanzibar na pia matumizi ya Sheria ya Mitandao kwenye Uchaguzi Mkuu uliopita. Tanzania inasubiri kiasi cha Dola milioni 472 za Marekani (sawa na zaidi ya Sh. trilioni moja) kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo.
Hata hivyo, nchi yetu imejikuta njia panda kutokana na suala la Zanzibar ambalo lilikumbushwa na uongozi wa MCC.
MCC baada ya kikao chake mwezi uliopita, ilionya kuwa itakuwa ngumu kwa Tanzania kupata fedha hizo ikiwa suala  la Zanzibar halitapatiwa ufumbuzi.
Pia tukio la kukamatwa kwa watu mbalimbali kwa makosa ya mitandao wakihusishwa na ukusanyaji na ujumlishaji wa matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba, ni sababu nyingine ya kukosa msaada wa MCC.
MCC ilisema inahusisha mambo hayo na utawala bora na suala la uhuru wa kujieleza na kuitaka Tanzania kushughulikia mambo hayo kama inataka ipate fedha za MCC.
Tunaiomba serikali iongeze jitihada za kuutatua mgogoro wa Zanzibar kwani kwa kiasi kikubwa unaitia doa nchi yetu kwenye medani ya kimataifa.
Tanzania ni miongoni mwa mataifa yanayosifika duniani kwa kudumisha amani na utulivu miongoni mwa raia wake.
Ndiyo mara nyingi imehusishwa na jitihada mbalimbali za kutatua migogoro mbalimbali ya kimataifa.
Tanzania imewahi kuhusika katika kusuluhisha migogoro mingi kama ya Burundi, Sudan Kusini, Rwanda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Watu wengi wanajiuliza imekuwaje mgogoro wa Zanzibar umeshindikana? Imefika wakati kwa viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutafuta suluhisho la kudumu la kumaliza tatizo la Zanzibar. Katika miaka ya karibuni, kila mara kumekuwa kukiibuka mgogoro kati ya CCM na CUF baada ya uchaguzi. 
Mgogoro wa safari hii uliibuka baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, Jecha Salim Jecha, kuamua kufuta matokeo ya uchaguzi wa Zanzibar.
Ndiyo maana tunapongeza hatua ya Rais Magufuli, lakini tunaomba wanasiasa wa Zanzibar waelewe kuwa mgogoro huu kwa kiasi kikubwa umeanza kuiumiza Tanzania.
Wanasiasa wanaohusika na mgogoro huu wanapaswa kutanguliza maslahi mapana ya taifa wakati wakishughulikia mgogoro huu.
Pia tunamshauri Rais Magufuli kuhimiza pande zote zinazohusika kufikia muafaka kwa kuzingatia maslahi mapana ya taifa. Hata hivyo, kubwa ni haki inatakiwa kutendeka kwa demokrasia kuheshimiwa kwa kuzingatia kanuni na sheria za uchaguzi wa Zanzibar kutokana na ukweli kuwa wananchi wa Zanzibar wana haki ya kuongozwa na viongozi wanaowataka.
Bila shaka jitihada hizi za Rais Magufuli zitazaa matunda ili kuwapatia nafasi wananchi wa Zanzibar kupumua na kuendesha maisha yao ya kila siku kwa amani na utulivu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment