Image
Image

Manahodha wa Stars walaani maamuzi ya Cannavaro’ kujiuzulu.

WACHEZAJI mbalimbali wa soka waliopata kuwa manahodha wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ wamezungumzia hatua ya nahodha wa timu hiyo Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kujiuzulu kuchezea timu hiyo, huku baadhi wakimshauri afute uamuzi wake.
Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Mecky Maxime amemtaka Cannavaro kufuta uamuzi wake wa kujiuzulu Taifa Stars kwani mchango wake unahitajika.
Maxime ambaye aliwahi pia kuwa nahodha wa Stars wakati ikiwa chini ya Mbrazil, Marcio Maximo, alisema alichofanya beki huyo si sahihi.
Hivi karibuni kocha wa Stars, Charles Mkwasa alimpa unahodha mchezaji wa TP Mazembe ya Congo DR Mbwana Samatta na kusema Haroub atabaki kuwa nahodha kwenye timu inayoshiriki michuano ya ndani ya Afrika (Chan).
Akizungumza na gazeti hili jana, Maxime alisema suala la unahodha mwenye uamuzi ni kocha, hivyo Cannavaro hana budi kukubaliana na maamuzi hayo na kwa nafasi anayocheza kwa sasa timu ya taifa bado anahitajika.
“Kwa nafasi ya mabeki wetu, Cannavaro bado anahitajika sana kwenye timu, arudi tu mchango wake bado unahitajika sana ingawa kujiuzulu ni utashi wake mwenyewe, lakini anahitajika bado ana uwezo na ana nidhamu nzuri,” alisema.
Akifafanua zaidi suala la nafasi ya nahodha, Maxime alisema: “Suala la kocha kumnyang’anya unahodha Cannavaro inaweza kuwa si sahihi au sahihi, yote kwa yote. “Sahihi kwasababu kocha ndio anaamua nani awe nahodha, kwani wachezaji wake anawafahamu vizuri, lakini pia unahodha hauna barua unajua maana hayo ni maamuzi ya kocha, mimi nadhani Cannavaro aelewe tu na si kweli kwamba amedharaulika,” alisema.
Naye nahodha mwingine wa zamani wa Taifa Stars, Peter Manyika ameungana na Maxime kwamba mchezaji huyo wa Yanga anapaswa kufanya kazi yake kwani uamuzi wa kuteua nahodha ni wa kocha.
“Kocha ndio anateua nahodha kwa sababu ndio bosi kwa hiyo kama ameamua basi atakuwa na sababu za msingi na hatuwezi kumuingilia sababu zake,” alisema.
Kuhusu kujiuzulu kwa Cannavaro, Manyika alisema hilo ni jambo la utashi wa mtu ingawa upande wake anaamini bado alistahili kuwepo kwenye timu.
“Kujiuzulu kila mtu ana upeo wake, unahodha unajua ni kitu kizito labda sababu za kuvuliwa kwake hazijamridhisha hatuwezi kujua kinachotakiwa hapo ni suluhisho ambalo naamini litafanywa na kocha na mchezaji mwenyewe,” alisema Manyika.
Tangu kufanyika kwa maamuzi hayo Cannavaro amekuwa akilalamika kwenye vyombo vya habari kwamba hakutendewa haki kwa namna alivyovuliwa unahodha. Lakini Mkwasa akizungumza na gazeti hili, alisema hajamvua unahodha Cannavaro bali alichokifanya ni mabadiliko ya kawaida kwenye timu.
“Sikuwa na sababu ya kumuondoa kwenye unahodha, namheshimu sana Cannavaro (Haroub) na ametoa mchango mkubwa kwa taifa hili na bado namhitaji, kwa nini nimuondoe,” alisema.
“Nilichokifanya ni mabadiliko kidogo tu kwenye kazi ni kama nyinyi huko kuna Mhariri wa Habari na Mhariri wa Michezo, ndivyo nilivyofanya mimi na hili lipo duniani kote, hata ukiangalia wenzetu Ivory Coast, Cameroon Zambia, Uganda na hata Rwanda… “Sasa hivi kuna mashindano ya Chan yanaendelea lazima utakuta nahodha wa Afcon sio yule wa Chan,” alisema.
Beki huyo ametangaza kujiondoa Taifa Stars kutokana sababu mbalimbali lakini mojawapo ikiwa ni kuvuliwa unahodha bila kupewa taarifa, ingawa kocha alisema alimjulisha.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment