Image
Image

Kasi ya TRA kukusanya mapato iwe endelevu isiishie hapo.

GAZETI hili jana lilichapisha habari iliyokuwa na kichwa cha habari “TRA yakusanya Shilingi trilioni 1.7 kwa mwezi.”
Hii ni kazi nzuri inayofanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kuonesha kwa uwazi uhalisia wa makusanyo hayo kutoka kwa walipa kodi.
Tulizoea kusikia hesabu ya mamilioni na bilioni, lakini kwa kasi na juhudi mpya tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli, kuna kila dalili ya kusahau makusanyo ya mamilioni na bilioni na kwenda katika hatua nyingine ya trilioni, lugha ambayo imeanza kuzoeleka na kusikika kwenye masikio ya watanzania wengi, tofauti na hapo awali.
Hakuna ubishi kwamba matunda hayo ya trilioni, tunazosikia zinatokana na juhudi za wazi na za makusudi ya dhamira ya serikali ya kuhakikisha mapato, yanakusanywa kwa umakini mkubwa kwa kumhusisha kila anayestahiki kulipa kodi anafanya hivyo, ikiwa ni pamoja na wafanyakazi ambao mara nyingi uwezekano wa kukwepa kulipa kodi huwa ni mdogo.
Wote ni mashahidi kwamba kasi mpya ya kuziba mianya ya wakwepa kulipa kodi kutoka bandarini, TRA na wafanyabiashara wasio waaminifu ndiko kunakotufikisha katika hatua hii ya mafanikio ya kufikia makusanyo ya trilioni.
Tunapenda kuchukua fursa hii, kuwapongeza wenzetu wa TRA na serikali kwa ujumla wake, kwa kulivalia njuga suala hili nyeti kwa uhai na ustawi wa watanzania wote kwa kukusanya kodi kwa mujibu wa sheria na taratibu.
Tuna imani kwamba hali ya makusanyo, itaendelea kung’ara kwa miezi ijayo, ukizingatia kwamba Jeshi letu la Polisi limerejeshwa tena katika Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), kuhakikisha kwamba mianya iliyotumika na wajanja wachache kuhujumu makusanyo, ikiwa ni pamoja na makontena kwa maelfu kuondolewa bandarini bila kulipia kodi, sasa itadhibitiwa ipasavyo.
Sote ni mashuhuda kwa habari tuliyochapisha jana, iliyomkariri Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dk Silvarius Likwelile akieleza kuwa fedha zilizokusanya, zimekwishasambazwa kulipia huduma mbalimbali za jamii kwa mabilioni.
Miongoni mwa maeneo ambako mabilioni hayo yamepelekwa ni Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), utoaji wa elimu bure, mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, kuwajengea uwezo walimu, mipango ya maji vijijini, ujenzi wa barabara, miradi ya umeme vijijini, maendeleo ya mahakama na upanuzi wa udahili wa wanafunzi kwa mkoa wa Dar es Salaam.
Tunadiriki kusema kwamba haijawahi kutokea serikali ikatoa mabilioni ya fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa kiwango cha mabilioni na kwa uwazi kiasi hiki. Tumefikia hatua hiyo kubwa kutokana na makusanyo ya uhakika ya kodi. Kinyume chake, tungekuwa tunaendelea kusubiri wahisani wa kutupatia misaada.
Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Magufuli imeshatamka wazi kwamba haitaki kuwa ombaomba kutokana na ukweli kwamba nchi imejaliwa rasilimali za kutosha.
Iwapo tutatumia rasilimali hizo kwa umakini na kwa uadilifu na kuchapa kazi bila kufanya ajizi, ikiwemo kujenga viwanda na kutumia vizuri rasilimali za gesi na mafuta, Tanzania itaweza kuingia katika uchumi wa kati hivi karibuni. Tusikubali kurudi nyuma. Tuendelee kupambana. Mungu Ibariki Tanzania.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment