Image
Image

Simbachawene kutumbua majipu ya wakurugenzi wa halmashauri nchini.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene amesema kuwa wakurugenzi wa halmashauri nchini, wakaoshindwa kutekeleza agizo la kujitosheleza kwa madawati katika shule ya msingi na sekondari hadi Juni mwaka huu, wajitambue wameshindwa kazi.
Pia wakurugenzi wa halmashauri watakaozalisha madeni ya watumishi pamoja na ya wazabuni wa vyakula katika shule za serikali, watakuwemo kwenye kundi la kuwajibishwa.
Waziri huyo wa Tamisemi alitoa kauli hiyo juzi wakati akizungumza na Viongozi wa Serikali ya Mkoa wa Morogoro wakiwemo wakuu wa wilaya, wakurugenzi watendaji wa halmashauri (Ma-DED), makatibu tawala wa wilaya, na wakuu wa idara za halmashauri zote za mkoa huo chini ya Mkuu wa Mkoa, Dk Rajab Rutengwe.
Hivyo alisema agizo lililotolewa na Rais John Magufuli la kutaka kuona kila mwanafunzi anaketi kwenye madawati, halina mjadala na kwamba ifikapo Juni mwaka huu pasiwepo na mwanafunzi anaketi sakafuni na wakurugenzi watakaoshindwa, watakuwa wameshindwa kazi na watawajibishwa.
Aliagiza wakuu wa mikoa na wilaya, ambao ndiyo wasimamizi wa rasilimali zilizopo katika maeneo yao hasa ya misitu, wasisite kutoa vibali vya uvunaji wa miti ya kutengeneza madawati kwenye wilaya zao ili watoto wote waliopo shuleni wawe wanakaa kwenye madawati.
“Tumieni vyema nafasi zenu za kuwa wenyeviti kamati za kutoa vibali vya uvunaji rasilimali za misitu... ili madawati yaweze kupatikana na utekelezaji wa matumizi ya vibali hivyo ufuatiliwe ili visitumiwe vibaya na waliopewa kazi hizo,” alisema Waziri.
Alitoa mfano kuwa Mkoa wa Morogoro ambao una rasilimali nyingi za misitu, umekuwa na upungufu wa madawati ni 73,972 katika shule za msingi na 11,038 katika shule za sekondari za serikali.
Pia alisema mkoa una upungufu wa vyumba vya madarasa 4,508 kwa shule za msingi na madarasa 352 kwa shule za sekondari za serikali wakati eneo la afya lina upungufu wa zahanati 334.
“Kuna kazi kubwa katika sekta ya elimu ambapo kwa Mkoa wa Morogoro pekee unakabiliwa idadi ya madawati mengi sembuse wilaya kama ya Kibaha,” alisema.
Waziri Simbachawene pia alionya tabia ya uzalishaji wa madeni ya watumishi wa halmashauri na wazabuni, wanaotoa huduma ya vyakula shule za serikali unaofanywa na watumishi wa Idara ya Uhasibu na maofisa utumishi kuwa siku zao, zinahesabika na wajiandae kutumbuliwa majipu.
Ili kutekeleza agizo la kukomesha uzalishaji wa madeni, alitoa maelekezo kwa maandishi kwa wakurugenzi wa halmashauri zote 181 kwa ajili ya utekelezaji wake.
Alisema halmashauri hizo, zina uwezo wa kulipa madai ya wafanyakazi wake kama nauli ya likizo, gharama za matibabu na mambo mengine kwa kutumia fedha za makusanyo yake ya ndani kwa kuwa fedha za mishahara na mengine zinatolewa na Serikali Kuu.
“Serikali inalaumiwa kwa sababu wakurugenzi hawatekelezi wajibu wao na matatizo mengi yapo katika Idara ya Uhasibu na Idara ya Utumishi,” alisema na kuongeza: “Wahasibu ni chanzo cha matatizo yote haya wanakuwa na mahusiano na wenye kutoa huduma, utakuta deni la shilingi bilioni 25 likihakikiwa linabakia shilingi bilioni tano, zimeongezwa tarakimu hapo na haya yameshatokea.”
Aliongeza, “Hawa sasa wajiandae kutumbuliwa, tunaelekea ngazi ya wakuu wa idara wa halmashauri, akitumbuliwa mkurugenzi naye mkuu wa idara anayehusika na kashfa hiyo atawajibishwa si kwa mkurugenzi pekee.”
Aliwakumbusha wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi wa halmashauri nchini kutambua jukumu walilopewa la ukamilishaji wa vyumba vya maabara na wasiokamilisha hicho ni mojawapo ya kigezo cha kupoteza nafasi zao.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment