Image
Image

Tuweke visingizio kando tuhamie Dodoma.

SERIKALI ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Rais, John Magufuli imeweka bayana kwamba itahamia Makao Makuu ya nchi, mjini Dodoma ndani ya miaka minne iliyobaki.
Rais Magufuli ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, alitoa msisitizo huo jana kwenye viwanja vya Mashujaa mjini Dodoma alipokuwa anawasalimia wakazi wa mji huo na Watanzania kwa ujumla wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mashujaa.
Tunapenda kumpongeza Rais katika salamu zake kwa kutoa angalizo kwamba atahakikisha serikali yote inahamia Dodoma bila kukosa na kuwataka viongozi wengine kuacha kutoa visingizio.
Pongezi hizo tunapenda pia zimwendee Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye alipopewa nafasi ya kuzungumza katika tukio hilo naye kwa upande wake alitangaza kuwa atahamishia ofisi yake mjini Dodoma mwezi Septemba, mwaka huu.
Waziri Mkuu hakuishia hapo pia aliweka bayana kuwa akishatangulia kwenda Dodoma, mawaziri wote na manaibu wao, nao watamfuata.
Ama kweli Hapa kazi Tu! Hakuna ubishi kwamba awamu zote zilizotangulia zilikuwa na mikakati mbalimbali ya kutaka kuhamia makao makuu ya nchi mjini Dodoma lakini sote ni mashuhuda kwamba azma hiyo haikutimizwa kutokana na sababu mbalimbali.
Sisi tunapenda kurudia pongezi zetu kwa Rais wa Awamu ya Tano na Serikali yake, kwa kulivalia njuga jambo hilo na kusisitiza kuwa lazima kuhamishia mawazo hayo katika vitendo. Hapa tunapenda kutoa mwito kwa wananchi,viongozi wa siasa na serikali kila mmoja kwa nafasi yake kutoa kila aina ya ushirikiano na mshikamano ili sote kwa pamoja kuhakikisha kwamba azma hii inatekelezwa bila kufanya ajizi.
Harakati zozote za kudhoofisha mkakati huo muhimu kwa Taifa letu zisipewa nafasi wala kusiwepo na kisingizio chochote kile kama Rais mwenyewe alivyofafanua katika salamu zake. Jambo moja la muhimu hapa ni kwamba atakayejaribu kwa namna yoyote ile kudhoofisha juhudi hizo afichuliwe kwenye vyombo husika ili adhibitiwe kwa mujibu wa sheria na taratibu.
Kwa wakazi wa Dodoma, huo sasa ni wakati wa kujiandaa kwa maana ya kuwa tayari kwa kuzipokea kwa mikono miwili fursa zinazokuja mbele yao kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kisiasa. Wakazi wa Dodoma wasiwe watazamaji bali wawe washiriki kikamilifu katika ujenzi wa miradi mikubwa ya hoteli za kisasa, nyumba za kupangisha na kufikia wageni, utalii, migahawa na maeneo ya burudani.
Hakuna ubishi kwamba Dodoma ya miaka minne ijayo itakuwa na utofauti wa aina yake katika nyanja zote za kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni. Masuala ya kuboresha miundombinu ili iendane na mahitaji ya idadi ya watu na ofisi za serikali na watumishi wake nayo yana umuhimu wa pekee.
Barabara ziboreshwe kwa viwango vya lami, usambazaji wa umeme, maji na masoko navyo vipewe kipaumbele kinachostahiki ili kutekeleza kwa ufanisi zoezi zima la serikali nzima kuhamia Dodoma. Hayo yote yanawezekana tujipange kuyatimiza.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment