Image
Image

Serikali yaiagiza (TANROADS), kuondoa matuta kwenye barabara kuu.

Serikali imeagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), kuondoa matuta kwenye barabara kuu, ambayo yametajwa kuwa chanzo cha ajali.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni, ametoa agizo hilo jana wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Usalama Barabarani katika Viwanja vya Kalangalala mkoani Geita.
Alisema matuta yaliyoko kwenye barabara kuu, yamekuwa moja ya vyanzo vya ajali nyingi nchini na kusisitiza kuwa hali ya ajali iliyopo ni vyema suala la usalama barabarani kuwa ajenda ya kitaifa.
Pia alivitaka vvyombo vya usalama, kuwachukulia hatua kali na stahiki wale wote wanavunja sheria za Usalama Barabarani bila kumuogopa au kumuonea mtu yeyote.
Alisema ajali za barabarani zimekuwa ni tatizo kubwa na kuwa takwimu za miaka mitatu kuanzia Januari 2013 hadi Desemba 2015, zinaonesha kuwa ajali zilizotolewa taarifa ni 46,536 ambazo zimeua watu 11,230.
Masauni alisema kuwa kundi linaloongoza kwa kuathirika na ajali hizo ni abiria ambapo watu 3,444 wamekufa, wakifuatiwa na watembea kwa miguu 3,328.
Alisema wapanda baiskeli wanashika nafasi ya tatu kwa watu 2,493 kupoteza maisha, huku madereva waliokufa ni 813 na wasukuma mikokoteni zaidi ya 400 wamepoteza maisha.
“Takwimu za miezi sita tangu Januari mpaka Agosti mwaka huu, ajali 6,971 zimetokea na kusababisha vifo 2,217 na kati ya hivyo 1,809 ni vile vilivyotokana na pikipiki. Hali ya ajali sio nzuri na ni vyema suala la usalama barabarani likawa ajenda ya kitaifa,” alisema.
Alisisitiza kutolewa elimu ya watumiaji wote kuhusu matumizi sahihi ya barabara, wamiliki na madereva kuacha kuendesha vyombo chakavu na kufanyika kwa ukaguzi wa mara kwa mara.
“Shirika la Viwango Tanzania (TBS) pia linatakiwa kuendelea kufanya ukaguzi wa matairi, bodi na vipuri vya mabasi,” alisema.
Aidha, Masauni aliwataka watumiaji wote wa barabara, kufuata sheria na kanuni za barabarani, kuacha kushabikia mwendo kasi, kuvuka kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na waendesha baiskeli na mikokoteni kuacha kuendesha barabarani na watoto kuvuka barabara wakiwa chini ya uangalizi.
Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, Edwin Ngonyani, alisema kutokana na kukithiri kwa ajali, Baraza lilikuja na mikakati ya miezi sita ya kupunguza ajali hususan zinazotokana na makosa ya kibinadamu.
Alisema makosa ya kibinadamu yamekuwa yakichangia ajali kwa asilimia 80 na kufuatiwa na mwendokasi ambao unachangia kwa asilimia 12, mazingira ya barabara yanachangia kwa asilimia 6 na asilimia 2 zinatokana na sababu nyingine.
“Tumekuja na mikakati ambayo inatekelezwa kwa miezi sita, lengo kuu ni kuondoa makosa ya kibinadamu yanayochangia ajali, na Februari mwakani tutatathmini mafanikio ya mikakati hiyo,” alisema.
Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani katika Jeshi la Polisi, Mohammed Mpinga, ambaye pia ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, alisema katika Wiki ya maadhimisho hayo watoa elimu ya matumizi sahihi ya barabara, na kutoa elimu kwa waendesha pikipiki 300 na walimu 100, na pia watakagua vyombo vya moto na kupima afya za madereva kwa kutumia zahanati mwendo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment