Image
Image

MAMLAKA ya Mapato nchini (TRA) yazua tafrani TFF.

MAMLAKA ya Mapato nchini (TRA), kwa kushirikiana na Kampuni ya udalali ya Yono Action Mart jana iliibuka tena kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), na kuzua tafrani kubwa kwa kutaka kufunga ofisi hizo kutokana na kudaiwa deni la Sh bilioni 1.6. Maofisa hao wa TRA wakiongozana na lundo la madalali wa Yono walitinga ofisi hizo za TFF zilizopo Karume, Ilala saa nane mchana kuanza kufunga mageti na baadhi ya magari yaliyokuwa yameegeshwa kwenye ofisi za shirikisho hilo huku wahusika wa magari hayo wakitakiwa kutoka kwa kitambulisho ili kujua magari yanayomilikiwa na TFF.
HabariLeo ilikuwepo kwenye ofisi hizo na kushuhudia kila kilichoendelea.
Hata hivyo Katibu Mkuu wa TFF, Selestine Mwesigwa aliwaomba maofisa hao wa TRA kuzungumza na baada ya mazungumzo ya muda mrefu kidogo TRA na Yono wakaondoka kwa makubaliano kuwa TFF watamalizana nao leo hadi kufikia saa nne asubuhi.
Meneja Operesheni wa Yono, Kasimir Mwandema alisema kuwa wanachofanya wao ni kutekeleza agizo la TRA kwa kukamata mali za TFF ili kufidia deni la Sh bilioni 1.6.
“Walitakiwa wawe wameshamaliza kulipa deni kwa mujibu wa makubaliano ya awali waliyoomba, lakini mpaka sasa hakuna kilicholipwa," alisema Mwandema huku madalali hao wa Yono wakizingira ofisi hiyo wengine wakiwa ndani na wengine wakiwa nje na kuzuia magari ya watu ambao walifika kwa ajili ya huduma mbalimbali.
Hata hivyo, baada ya tafrani iliyodumu takribani nusu saa na kuzua taharuki kwa wafanyakazi wa shirikisho hilo, hatimaye TFF waliahidi kumalizana na TRA leo.
“TFF wameomba wakae na TRA wamalizane, tumewapa leo (jana) mpaka kesho (leo) saa tatu asubuhi, kufanya hivyo, kuanzia saa nne tupo hapa kama hawatamalizana hatutakuwa na jinsi zaidi ya kutekeleza agizo tulilopewa,” alisema.
Alisema TRA imekuwa ikiwadai Sh bilioni 1.118 ambayo ni kodi mchanganyiko kuanzia mwaka 2010 hadi 2015, kodi hizo VAT, Kodi ya Mapato, SBL na kwamba hapo nyuma walikamata akaunti zao kwa sababu deni lilikuwa ni Sh bilioni 1.6 na wakapunguza sehemu ya deni lakini halijaisha ndio sababu wanataka kukamata tena mali za TFF.
Hii ni mara ya tatu kwa mwaka huu TRA kuvamia ofisi za TFF na kukamata mali zake, Machi ilizuia fedha za TFF kwenye akaunti zake na baadaye ikakamata magari matano ya shirikisho hilo ikiwemo basi la timu ya taifa, Taifa Stars.
Hata hivyo Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa hakuwa tayari kuzungumzia suala hilo, na baada ya maofisa hao wa TRA na Yono kuondoka, aliitisha kikao cha dharura kwa baadhi ya watendaji ikiwemo Idara ya Uhasibu kujadili suala hilo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment