Image
Image

MIKUTANO YA UTATU YA KANGANYA WANACHAMA WA JUMUIA YA AFRIKA MASHARIKI ( EAC )


Mkurugenzi wa Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii toka Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. George Lauwo(kushoto) Akifafanua kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mchakato kuelekea matumizi ya mfumo mmoja wa fedha, wakati wa Mkutano uliofanyika ukumbi wa idara ya habari(MAELEZO) Jijini Dar Es Salaam,Kulia ni Mkurugenzi wa Siasa,Ulinzi na Usalama Bw. Steven Mbundi.

Mkuu wa kitengo cha mawasiliano toka Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Vedastina Justinian(kushoto) akieleza kwa waandishi wa habari(Hawapo pichani)kuhusu Mikutano ya utatu kati ya Nchi za Kenya, Uganda na Rwanda,wakati wa Mkutano uliofanyika ukumbi wa idara ya habari(MAELEZO) leo Jijini Dar Es Salaam. Kulia ni Afisa Habari wa Idara ya Habari(MAELEZO) Fatma Salum.
...........................................................................................



Na.Mwandishi Wetu.
Hivi karibuni wananchi wengi wamekuwa wakifuatilia na kuulizia kuhusu taarifa mbali mbali zinazotolewa na vyombo vya habari juu ya hatua ya baadhi ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) za Kenya, Uganda na Rwanda kufanya mikutano ya utatu kujadili masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki pasipo kuzishirikisha nchi za Tanzania na Burundi. 

Mikutano hiyo inaandaliwa kupitia utaratibu wa Ushirikiano wa nchi hizo tatu kupitia Wizara za Mambo ya Nje ya Nchi zao na sio kupitia mfumo wa Sekretariati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kulingana na taarifa zilizotolewa kwa vyombo ya habari mara baada ya kukamilika kwa mkutano wa wakuu wa nchi hizo tatu uliofanyika tarehe 24-25 Juni, 2013 huko Entebbe Uganda. Masuala yaliyojadiliwa na kutolewa maamuzi na  mwongozo wa utekelezaji ni pamoja na:

Ujenzi wa Reli ya Kisasa kutoka Mombasa-Kampala– Kigali Km 2,784;
Ujenzi wa Bomba la Mafuta South Sudan-Kampala-Kenya;
Ujenzi mitambo ya kusafisha mafuta  Uganda;
Kuongeza upatikanaji wa Umeme;
Kuanzisha  Himaya Moja ya Forodha; (single customs Territory)
Kuharakisha Shirikisho la Kisiasa;
Vitambulisho vya Kitaifa kutumika kama Hati ya Kusafiria; na
Visa ya Pamoja ya Utalii.

UFAFANUZI.

Pamoja na kuwa Ibara ya 7(1) (e) ya Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), inaruhusu nchi wanachama kuwa na Ubia (Bi-lateral or Tri-lateral agreements), ni lazima suala linaloenda kutekelezwa chini ya mfumo huo liwe limejadiliwa na kukubalika na nchi zote wanachama.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mkutano wa 27 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki uliofanyika Arusha tarehe 31 Agosti, 2013, ilitaka kujua hatma ya mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. 

Tanzania ilitaka ufafanuzi kutokana na ukweli kwamba baadhi ya mambo ambayo nchi hizo zinayajadili na kuyatolea maamuzi, bado majadiliano yake yanaendelea katika ngazi ya Jumuiya. 

Baraza la Mawaziri la Afrika Mashariki lilimtaka Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri kutoa taarifa ya kina kuhusu mikutano hii na athari zake katika Mkutano wa 28 wa Baraza la Mawaziri unaotarajiwa kufanyika mwezi Novemba, 2013.

KUHARAKISHA UUNDWAJI WA SHIRIKISHO LA KISIASA

Katika moja ya mikutano hiyo, Wakuu wa Nchi za Kenya, Uganda na Rwanda walikubaliana kuharakisha uundwaji wa Shirikisho la Kisiasa baina ya nchi hizo tatu.

Ibara ya 5(2) ya Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki imeainisha hatua za mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kuwa ni Umoja wa Forodha, ukifuatiwa na Soko la Pamoja, kisha Umoja wa Fedha,  na hatimaye Shirikisho la Kisiasa.

Kuanzia mwaka 2004 kumekuwa na jitihada mbali mbali za kutaka kuharakisha uundwaji wa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki. Hii pamoja na hatua nyingine mbali mbali ilipelekea kuundwa kwa Timu za Kukusanya Maoni ya Wananchi juu ya pendekezo hilo. 

Kwa upande wa Tanzania iliundwa timu iliyokuwa na chini ya Uenyekiti wa Professa Samweli Wangwe na matokeo yaliyoonyesha kuwa asilimia 79.4 ya watanzania hawataki kuharakisha uundwaji wa shirikisho. Serikali ya Tanzania daima inazingatia maoni haya ya wananchi.

Ili kuwawezesha wananchi kujua aina ya shirikisho linalotarajiwa kuundwa, Wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya waliiagiza Serikali ya Jumuiya kuunda Rasimu ya Modeli ya Shirikisho. Na kwa sasa nchi wanachama wanafanya mashauriano ya ndani kuhusiana na rasimu iliyowasilishwa.

VITAMBULISHO VYA KITAIFA KUTUMIKA KAMA HATI YA KUSAFIRIA.

Itifaki ya Soko la Pamoja Ibara ya 9(2) Nchi Wanachama zilikubaliana kutumia hati halali za kusafiria (Passport) katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.  

Hati hizo ni Passport ya Nchi Mwanachama na Passport ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Aidha, imekubalika pia kuwa Nchi Wanachama ambazo zipo tayari kutumia vitambulisho vya uraia kama hati za kusafiria zinaweza kuendelea kwa kufanya makubaliano baina yao ili mradi tu vitambulisho hivyo viwe machine readable.

KUANZISHA HIMAYA MOJA YA FORODHA

Mwaka 2012 Wakuu wa Nchi Wanachama waliridhia uanzishwaji wa Himaya Moja ya Forodha inayotaka bidhaa zinazopitia nchi moja kuelekea nchi nyingine mwanachama kukaguliwa na kodi kukusanywa katika kituo cha forodha cha kwanza bidhaa inapoingia katika Jumuiya. 

Masuala muhimu yanayojadiliwa ni pamoja na kuondoa dhamana (bond) kwa mizigo iliyolipiwa kodi, na matumizi ya njia ya kisasa ya ufuatiliaji wa misafara ya mizigo (electronic cargo tracking system) kama njia mbadala ya matumizi ya dhamana (bond); matumizi ya dhamana moja (single bond) kwa mizigo yote inayosafirishwa kwenda nje ya Jumuiya na mizigo ambayo haijalipiwa kodi.

HITIMISHO

Tanzania ni sehemu ya mtangamano na nia yetu ni kuhakikisha tunatekeleza makubaliano yetu ya pamoja kulingana na matakwa ya Mkataba wa Uundwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Imetolewa na:

WIZARA YA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment