Image
Image

Hatima na Ubunge wa Zitto waning’inia

Kitendo cha kutupiana mpira kati ya Ofisi ya Bunge, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuhusu hatima ya Zitto Kabwe, kimeufanya ubunge wa mbunge huyo kuendelea kuning’inia huku mwenyewe akitazamiwa leo kueleza anachoita ‘maamuzi magumu’.
Kutupiana mpira kulijitokeza jana baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kusema Bunge linasubiri taarifa rasmi ya kufukuzwa uanachama kwa mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini kutoka NEC, ambayo hata hivyo, nayo ilisema inasubiri taarifa kutoka Chadema huku chama hicho kikisema kinashughulikia kwanza kesi zinazowakabili wanachama wake wanaotuhumiwa kumpiga aliyekuwa mlinzi wa Katibu Mkuu wake, Dk Willibrod Slaa.

Wakati Makinda akieleza hayo, taarifa kutoka kwa watu wa karibu wa mbunge Zitto zilieleza kuwa leo ataibuka bungeni kwa nia ya kuwaaga wabunge kama alivyoahidi wiki iliyopita.

Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Zitto alishindwa kukubali wala kukataa, lakini akathibitisha kuwa atahudhuria kikao cha Bunge leo.

Chadema ilimvua Zitto uanachama wiki iliyopita saa chache baada ya Mahakama Kuu kutupa shauri lake alilofungua akitaka chombo hicho cha sheria kimlazimishe katibu mkuu wa chama hicho kumpa nyaraka za vikao vya Kamati Kuu vilivyomvua nyadhifa zote. Alipata amri ya muda ya kuizuia Chadema kumjadili.

Akifafanua suala hilo, Makinda alisema, “Unajua suala hili lilikuwa mahakamani, hivyo ni lazima tupewe taratibu zote za kimahakama. Kama kila kitu kikiwasilishwa moja wa moja uamuzi huo utatangazwa wazi. Unajua suala hili lipo wazi na sisi kama Bunge tunachokisubiri ni taarifa tu.”

Hata hivyo, alisema kwa muda uliobaki wa miezi saba kabla ya uchaguzi mkuu, haiwezekani ukafanyika uchaguzi mdogo katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, “Labda kama ingekuwa imebaki miezi 12 au zaidi kabla ya uchaguzi mkuu, hapo ungeweza kufanyika uchaguzi mdogo.”

Katika mkutano wake na waandishi wa habari alioufanya muda mfupi kabla ya kuwaaga wananchi wa jimbo lake Jumapili iliyopita, Zitto alisema hatima yake ya ubunge itajulikana wiki hii kama Bunge likipata taarifa za yeye kufukuzwa uanachama.

Alisema iwapo hatua hiyo itakamilika, ataeleza hatua ambazo atazichukua na kufafanua kuwa mpaka sasa hajapata barua ya wito wa kwenda kujitetea katika Kamati Kuu ya Chadema, hivyo mpaka sasa bado ni mwanachama wa Chadema.

Alisema ataendelea kuwatumia Watanzania akiwa mwakilishi wao kupitia jimbo lolote nchini na kusisitiza kuwa atatoa kauli iwapo atagombea ubunge katika jimbo lipi na kwa tiketi ya chama kipi cha siasa.

 Mkurugenzi wa NEC, Julius Malaba aliliambia gazeti hili jana kwa simu kwamba bado hawajapata taarifa ya maandishi ya kufukuzwa kwa Zitto, hivyo hawezi kuzungumzia suala hilo.

Gazeti hili lilipowasiliana na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema – Bara, John Mnyika kama chama hicho kimetoa taarifa za Zitto NEC kuhusu kuvuliwa kwake uanachama, alijibu kuwa viongozi wakuu wa chama hicho wanashughulikia kesi zinazowakabili wanachama wa chama hicho wanaotuhumiwa kumpiga aliyekuwa mlinzi wa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Slaa.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment