Image
Image

Dk.Shein:Kuongezeka kwa kasi makusanyo kupitia Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) ni uthibitisho kuwa Mamlaka hiyo inatekeleza majukumu yake ipasavyo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuongezeka kwa kasi makusanyo kupitia Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) ni uthibitisho kuwa Mamlaka hiyo inatekeleza majukumu yake ipasavyo.
 “Ni mabadiliko ya haraka sana katika ukusanyaji wa mapato kutoka jumla ya wastani wa trilioni 5.4 mwaka 2010/2011 hadi trilioni 9.8 mwaka 2013/2014 kwa nchi nzima. Tafsiri ya mabadiliko haya ni kuwa TRA inafanya vizuri” Dk. Shein amesema.

 Alitoa mfano kwa upande wa Zanzibar kuwa Mamlaka hiyo pia imeweza kuongeza ukusanyaji wa mapato kutoka bilioni 91.69 mwaka 2011/2012 hadi bilioni 136.7 mwaka 2013/2014 huku makusanyo ya mwaka 2014/2015 yakitarajiwa kuongeza kupita nwaka uliopita.

 Akizungumza na Bodi ya Mamlaka hiyo Ikulu leo, Dk. Shein amesema historia inaonesha kuwa kazi ya kukusanya kodi kote duniani ina vikwazo vingi hivyo aliwataka watumishi wa Mamlaka hiyo kutokata tamaa na changamoto zinazowakuta badala yake kuzitafuta ufumbuzi na kuongeza juhudi kazini.

 “changamoto zipo haziwezi kuondoka na ukweli ni kuwa hata wakati wa Mitume kazi ya ukusanyaji kodi ilikuwa ngumu kwa kuwa mfanyabiashara kama walivyo baadhi ya binadamu akipatacho hapendi kukitoa” 

 Aliwahakikishia wajumbe wa bodi hiyo walioongozwa na Mwenyekiti wake Bernard Mchomvu na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo Bwana Rished Bade kuwa Serikali zote mbili zinaridhika na utendaji wa Mamlaka hiyo na zinaamini kuwa itafikia malengo ya serikali ya kuanzisha mamlaka hiyo.

 Dk. Shein ameipongeza TRA kwa kubuni mikakati mbali mbali ya kuongeza mapato ya serikali lakini akahimiza maandalizi ya kutosha, uwazi na elimu kwa walengwa ambao ni walipa kodi.

 “Katika mipango yetu tunayoibuni kuongeza mapato ni muhimu kuzingatia uwazi kadri inavyowezekana kwa kuwa kukosekana kwa uwazi na elimu ya kutosha kwa walengwa kunaweza kusababisha matokeo yasiyotarajiwa” Dk. alieleza.

 Mapema akitoa maelezo kwa Mheshimiwa Rais, Mwenyekiti wa Bodi hiyo Bwana Bernard Mchomvu alisema Mamlaka hiyo imejidhatiti kukusanya kodi ili kukidhi mahitaji ya taifa na kwamba inachukua hatua mbali mbali kufikia malengo yake.

 “Ili tuweze tuweze kufikia malengo kukidhi mahitaji ya taifa tumepanga kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazotukabili ikiwemo kuweka mazingira mazuri ya kukusanya kodi kwa watumishi wa Mamlaka na mazingira mazuri ya watu kulipa kodi”alieleza Bwana Mchomvu.

 Alitaja baadhi ya vikwazo vinavyozuia kukusanya mapato mengi zaidi kuwa ni pamoja na ukwepaji kodi, uingizaji bidhaa kwa magendo, udanganyifu katika orodha ya bidhaa zinayoingia na misamaha ya kodi jambo ambalo hivi sasa Serikali inalishughulikia.

 Bwana Mchomvu alieleza umuhimu wa waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kushiriki katika kutoa elimu kwa walipa kodi ikiwemo matumizi ya mashine za kisasa za mauzo ambazo baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakizipinga.

 Alisema mashine hizo ni bora na zinamsaidia mfanyabiashara kuweka mahesabu yake vizuri lakini inaonesha wafanyabiashara wengi hawapendi mambo yao kujulikana.

 Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TRA Bwana Rished Bade alieleza kuwa hivi sasa Mamlaka hiyo inafanya mabadiliko kadhaa ikiwemo kuweka mfumo mpya wa forodha na ifikapo mwezi Juni mwaka huu mfumo huo utaanza kutumia Zanzibar.

 Aidha Mamlaka alisema itaongeza uwazi katika kupitisha viwango vya kodi ili walengwa wavifahamu mapema sambamba na kuongeza kasi ya utoaji wa elimu kwa walipa kodi.

 Aliongeza kuwa Mamlaka hiyo itaongeza nguvu pia katika kukabiliana na wakwepa kodi, itaajiri watumishi zaidi ili kuwafikia walipa kodi wengi zaidi pamoja na kuwabadili watumishi mara kwa mara kuepusha kuzoeleka katika eneo moja la kazi.

 Mamlaka alieleza Mkurugenzi Mkuu huyo kuwa ina mpango wa kuwapatia mafunzo zaidi watumishi wake ili waweze kuwa na uwezo mzuri katika kutathmini thamani ya bidha na kodi zake.

 Wajumbe hao wa Bodi ya TRA wako Zanzibar kuhudhuria kikao cha bodi hiyo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment