Image
Image

Vitendo vya ukiukwaji haki za binadamu vikomeshwe.


Kuna taarifa za kusikitisha kuhusiana na namna haki za binadamu zinavyozingatiwa nchini. Ripoti iliyotolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) inaonyesha kuwa vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu viliongezeka zaidi mwaka 2014 kulinganisha na miaka iliyopita.
Ripoti hiyo ilionyesha kuwa baadhi ya maeneo ambayo haki za binadamu zilikiukwa ni pamoja na vifo vya watu wasiokuwa na hatia, ambao waliuawa kwa sababu ya imani potofu za kishirikina. Ilionyesha vilevile kuwa safari ya kuelekea kilele cha demokrasia nchini bado ndefu kwani utekelezaji wa misingi ya dhana hiyo bado umekuwa ukikabiliwa na changamoto za kila namna.
Takwimu katika ripoti hiyo zilionyesha kuwa matukio ya vifo vinavyotokana na imani za ushirikina yaliongezeka kutoka watu 2,583 mwaka 2010 hadi  2,936 kufikia mwishoni mwa 2014. Ilibainishwa na ripoti hiyo vilevile kuwa watoto wa kike 1,302 walikeketwa mwaka 2014 katika mikoa ya Singida na Mara pekee, huku wanawake 2,878 wakifanyiwa vitendo vya ubakaji na wengi wao wakiwa ni wasichana wenye umri mdogo.
Ripoti hiyo ilionyesha vilevile kuwa taifa bado linakabiliwa na janga la kuwa na baadhi ya maofisa wa vyombo vya dola wanowaua raia na hivyo kukiuka misingi ya haki za binadamu. Mauaji ya polisi mwaka jana, yakiwamo yaliyotokea Mkuranga mkoani Pwani yametajwa vilevile katika ripoti hiyo kwamba yameleta madhara  kwani chombo hicho ndicho kinacholinda amani nchini. 
Kadhalika, ripoti hiyo ilienda mbali zaidi kwa kuonya kuwa hatua yoyote ya kusainiwa kwa miswada ya habari ya haki ya kupata taarifa na huduma za vyombo vya habari ili kuwa sheria itazika rasmi demokrasia nchini; ambayo pia ni dhana muhimu kuzingatiwa kwa haki za binadamu.
Kwa ujumla, yapo maeneo mengi yaliyoguswa na ripoti hiyo. Siyo nia yetu kutaka kuijadili ripoti hiyo yote. Bali, tunadhani kwamba jambo jema zaidi ni kwa Watanzania wote, pamoja na watu wote waliopewa dhamana katika kila taasisi zilizotajwa, kuhakikisha kwamba hatua madhubuti zinachukuliwa ili kuzuia ukiukwaji zaidi wa haki za binadamu.  Kwamba, kama ilivyopendekezwa ndani ya ripoti hiyo, serikali ihakikishe kuwa kila Mtanzania anapata haki mbalimbali muhimu za binadamu zikiwamo za afya, elimu, kulindwa, kuwa huru kuchagua viongozi wa kisiasa na kushiriki katika shughuli za siasa.
Kinyume chake, kama huduma hizo zitakuwa haziwafikii Watanzania kwa kiwango kinachotarajiwa, ni wazi kwamba haki za binadamu zitaendelea kukandamizwa na hilo halipaswi kuachwa liendelee kuwapo.
Kwa mfano, NIPASHE tunaamini kuwa uvunjifu wa haki za binadamu katika eneo la afya utapungua kwa kiasi kikubwa ikiwa yale yote yaliyomo katika Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (MMAM) yanazingatiwa. Mathalan, kama zahanati nyingi zaidi zitajengwa katika kila kata, na kama zahanati hizo zitapatiwa vifaa vyote muhimu pamoja na madakatari na wauguzi wenye sifa, ni wazi kwamba huduma za afya zitaimarika na mwishowe kupunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya vifo vitokanavyo na magonjwa yanayotibika.
Sisi tunaamini vilevile kuwa serikali na wadau wengine wa maendeleo wanaweza kuanzisha kampeni maalum ya kuelimisha umma juu ya madhara ya kukumbatia imani potofu za kishirikina, hasa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ambayo ndiyo hukumbwa zaidi na matukio ya kuuawa kwa watu wasio na hatia kutokana na imani hizo. Na hili linaweza kufanikiwa zaidi ikiwa viongozi wa dini watahusishwa ipasavyo. Hii ni kutokana na ukweli kuwa wao wana wafuasi wengi na pia wana nguvu kubwa ya ushawishi, hasa kwa kutumia vifungu mbalimbali vya maandiko yanayokataza watu walio wema kujihusisha na mambo ya ushirikina.
Aidha, namna nyingine nzuri ya kukabiliana na vitendo vya kukiuka haki za binadamu ni kuhakikisha kuwa sheria za nchi zinapewa nafasi yake. Kwa mfano, kuishi ni haki ya kila mtu. Kamwe kusiwe na huruma dhidi ya watu wanaochukua sheria mikononi mwao kwa kuwaua watu wengine kutokana na tuhuma. Badala yake, wahusika wafikishwe kwenye mkono wa sheria ambako huko ndiko mahala pekee ambako haki hutolewa. Shime, vitendo vya ukiukwaji haki za binadamu vikomeshwe.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment