Image
Image

Simba yafuata majembe Brazil.

Klabu ya soka ya Simba itatinga nchini Brazil kwa ajili kutafuta wakali wapya wa kuimarisha kikosi hicho  kilichodhamiria kupigania ubingwa wa Ligi Kuu ya Bara msimu ujao utakaoanza Agosti 22, mwaka huu.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspoppe,aliiambia NIPASHE jana kwamba atakwea 'pipa' kesho kuelekea Brazil kwa ajili ya kusaka nyota wapya. 

Simba hadi sasa ina wachezaji wawili tu wa kigeni, Mganda Emmanuel Okwi na beki Juuko Murshid na imedhamiria kujaza nafasi zote saba, kama zinavyoruhusu kanuni mpya za ligi hiyo kuhusu wachezaji wa kigeni. Wakati dili la kumsajili mshambuliaji Mrundi, Laudit Mavugo, likionekana kuota mbawa, Simba tayari imeshaachana na nyota wake wa kimataifa, Danny Sserunkuma, Simon Sserunkuma na Joseph Owino huku Paul Kiongera akirejea Kenya kutokana na kutopona goti lake.

Hanspope alisema mbali na yeye kwenda Brazil, lakini pia wanapanga kutuma 'majeshi' Zimbabwe, Burundi na Uganda kwa ajili ya kusaka nyota zaidi wa kujaza idadi ya wachezaji saba wa kigeni. 

Aidha, Hanspoppe alisema kwa sasa hawezi kuthibitisha taarifa kwamba wanakaribia kumsajili mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Hamis Kiiza 'Diego'. 

Akizungumzia suala la kiungo, Ramadhan Singano 'Messi', alisema  bado wanamtambua ni mchezaji wao halali hadi mwakani na kwamba tayari wameshamlipia pango la nyumba ambalo mkataba uliisha na taarifa kuchelewa kuwafika, lakini sasa kila kitu kiko sawa. 

Kuhusu uvumi kwamba Singano anakwenda Azam, alisema analisikia tu, lakini halijafika mezani kwake. 

MZUNGU MWINGINE
Wakati kocha mkuu wa Simba Muingereza, Dylan Kerr, anatarajiwa kutangaza mikakati yake ya kiufundi ndani ya klabu hiyo kesho, uongozi wa klabu hiyo umesema kuwa leo utampokea kocha mpya wa viungo wa timu hiyo ambaye ni raia wa Serbia, Dusan Momcilovic.

Akizungumza na gazeti hili jana, Rais wa Simba, Evans Aveva, alisema kuwa kocha huyo wa viungo tayari ameshaingia mkataba mfupi wa mwaka mmoja na klabu hiyo na ajira yake itaanza sambamba kocha mkuu.

Aveva alisema kwamba ujio wa kocha huyo wa viungo utasaidia kuimarisha kikosi cha timu yao ambacho kinajiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara.

"Kocha wa viungo ataingia nchini kesho (leo) na mkataba wake unatarajia kuwa mfupi, awali tulitarajia kumpa mkataba wa mwaka mmoja, lakini inaweza kufikia mitatu kutokana na mahitaji yatakavyokuwa," alisema kiongozi mwingine ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Aliongeza kwamba Mserbia ana uzoefu mkubwa katika fani ya mpira wa miguu hususan mazoezi ya viungo.

Alitaja sehemu nyingine ambazo kocha huyo wa viungo amefanya kazi ni pamoja na Malaysia, Indonesia, Bosnia & Herzegovina, Oman na Georgia, ambako alikuwa kocha wa mazoezi ya viungo wa klabu ya FC Dinamo, iliyocheza mechi za awali za Ligi ya mabingwa Ulaya.

Kocha huyo pia amewahi kufanya kazi Afrika katika klabu ya FC SOGOR–Tobruk ya Libya na ana Digrii ya Mazoezi ya Viungo.

"Klabu ya Simba ina furaha kubwa kuingia mkataba na kocha Dusan Momcilovic mwenye uzoefu na weledi wa kutosha, tunaamini atakuwa chachu ya mafanikio pia katika kunoa vipaji vya wachezaji wa Simba," alimaliza Aveva.

Ujio wa kocha huyo unafanya idadi ya makocha wa kigeni ndani ya Simba kufikia watatu baada ya kocha wa makipa Mkenya, Abdul Iddi Salim na Kerr.

Simba ambayo ilishaanza mazoezi ya viungo chini ya kocha msaidizi, Selemani Matola, inatarajia kuingia kambini siku yoyote huku pia viongozi wakikamilisha mipango ya kwenda kuweka kambi Shelisheli.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment