Image
Image

CCM yaonyesha njia matumizi ya Tehama.

Mchakato wa uteuzi wa mgombea urais wa CCM umeonyesha dhahiri maendeleo ya matumizi ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), baada ya chama hicho kutumia mitandao ya kijamii kutoa habari muhimu za maendeleo ya mikutano yake iliyomalizika mjini Dodoma jana.
Taarifa za Kamati Kuu (CC), Halmashauri Kuu (NEC) na Mkutano Mkuu zilikuwa zikitolewa na chama hicho kwenye mitandao yake kabla hata ya kuzitangaza rasmi.

Tangu kuanza kwa mchakato wa mikutano hiyo, CCM ilionekana kujiandaa vilivyo baada kutumia karibu njia kuu zote za mitandao ya kijamii ikiwamo kurusha moja kwa moja matangazo ya Mkutano Mkuu kupitia kiunganishi cha mtandao www.bit.ly/MkutanoMkuu.

Licha ya kuwa chama hicho kilikuwa na akaunti za Facebook, Twitter, Youtube kwa muda mrefu, lakini kipindi hiki zilionekana kuboreshwa na kutumika mara kwa mara kiasi hata cha kutoa taarifa kabla ya Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye kuwatangazia wanahabari.

Ikumbukwe kuwa matokeo ya majina ya wagombea wa tano bora yaliwahi kutoka katika tovuti na akaunti ya Twitter ya chama hicho mara tu baada ya Kamati Kuu kumaliza kikao huku nyuma Nape akikwepa kuwaambia wanahabari.

Pia, matokeo ya tatu bora nayo yalitangazwa mapema kupitia vyombo hivyo dakika 10 mapema kabla ya Nape kuwatangazia rasmi wanahabari.

Hata hivyo, kasi ya vyombo hivyo kutangaza kile kinachoendelea kwenye mchakato huo ilitaka kuingia doa pale walipoandika kwenye ukurasa wao Twitter wenye jina @ccm_tanzania matokeo ya mshindi wa kinyang’anyiro cha urais na kuchanganya asilimia za kura walizopata wagombea Dk Asha Rose Migiro na Balozi Amina Salum Ali.

“Tunaomba radhi. Matokeo halisi ya kura za wagombea kutoka Mkutano Mkuu ni: Mh John Magufuli asilimia 87, Balozi Amina Ali asilimia 10, Dk Asha Migiro asilimia 3,” CCM ilisahihisha twiti yao baada ya kuandika kuwa Dk Migiro alikuwa amepata asilimia 10 na Balozi Amina asilimia 3.

Pia, CCM ilitumia nguvu kubwa kutangaza akaunti zake kwa kuziwezesha zionekane kwenye mtandao kwa kutumia reli #KaribuDodoma ambayo kwa mara ya kwanza ilionekana kuongoza kutajwa kwenye mtandao wa Twitter nchini.

Kwa kawaida, kuwezesha akaunti au neno lionekane mara kwa mara katika mitando ya kijamii unatakiwa kulipia fedha kutokana na mahitaji yako au watu waitaje mara kwa mara akaunti au neno hilo mtandaoni.

Awali, gazeti hili liliwahi kuzungumza na Nape juu ya mikakati ya kutumia Tehama wakati wa Uchaguzi Mkuu na kubainisha kwamba CCM ingetumia akisisitiza kuwa hiyo ni moja tu ya njia za kuwaunganisha na wananchi wenye uwezo huo lakini nguvu kubwa itaendelea kwenye mikutano ya hadhara inayowafikia hadi wananchi wa vijijini.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment