Image
Image

Tanzania ipo kwenye mikakati kukabili wizi wa fedha kwa kutumia mitandao.



Jitihada za Serikali katika kupambana na uhalifu wa mitandao imeungwa mkono kutokana na baadhi ya vyuo kuanzisha mitalaa yenye somo la ulinzi wa  mitandao.
Moja ya jitihada za serikali katika kukabiliana na changamoto hiyo ni kupeleka muswada wa sheria ya uhalifu wa mtandao ya mwaka 2015  katika mkutano wa 19 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao ulipitishwa na Bunge hilo.
Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknologia, Profesa Makame Mbarawa anasema, kukua kwa kasi kwa matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) kumeleta mafanikio kwa kuongezeka kwa biashara zinazotumia huduma za mawasiliano, fedha na matumizi ya mitandao.
Anaeleza kuwa hayo ni mapinduzi ya maendeleo kwa kutumia teknolojia lakini kwa upande mwingine yameleta changamoto nyingi katika jamii ikiwamo  kuibuka kwa uhalifu na kuibua makosa mapya ya jinai.
Makosa hayo, anasema yanajumuisha uhalifu wa mitandao ambapo simu za mkononi, kompyuta au mifumo ya kompyuta hutumika kama nyenzo za kutenda uhalifu huo.
Mifano ya makosa hayo ni pamoja na  wizi wa fedha kwa njia ya mtandao,  ugaidi,   maudhui potofu yanayosababisha mmomonyoko wa maadili,  uharibifu wa miundombinu muhimu ya Taifa ikiwamo mkongo wa Taifa wa Mawasiliano. 
Mtaalamu wa Ulinzi wa Mitandao, Ezekiel Mpanzo anasema tatizo la wizi wa mitandao limekuwa kubwa na kusababisha hasara kwa benki pamoja na wananchi.
Mpanzo ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Teknolojia na Uongozi cha Kilimanjaro, anasema  kwa upande wa vyuo vilivyopo chini ya Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) pamoja na vyuo vikuu wamegundua tatizo hilo na wamejaribu kutengeneza mtalaa ambao una somo la kuzuia wizi huo.
“Tumetengeneza mtalaa mzuri na kuingiza somo la ulinzi wa mtandao. Tumeuandaa sisi wenyewe na kuupeleka Nacte na wameupitisha, kwa hiyo tunaamini kwamba utasaidia Taifa kupunguza tatizo hilo,” anasema Mpanzo.
Anasema njia nyingine ya kuzuia tatizo hilo ni wataalamu wa hapa nchini kujiunga na vyama vya kuzuia uhalifu wa mitandao duniani. “Wataalamu wa hapa nchini, wakijiunga na vyama hivyo, vikiwamo Ethical Hacking na  Sisco, itasaidia kubadilishana uzoefu kuhusu mbinu wanazotumia wahalifu duniani kote kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknologia,” anabainisha Mpanzo.
Lengo lao, anasema ni nchi kuwa na wataalamu wengi watakaosaidiana na Serikali pamoja na taasisi mbalimbali, kukabili tatizo la wizi kwa kutumia mitandao.
Anasemakatika mwaka 2010 na robo ya mwaka 2013 Tanzania ilipoteza Sh9.8 bilioni kutokana na wizi huo ambao ulifanywa katika mashine za kutolea fedha maarufu kama ATM.
Hivi karibuni, Jijini Arusha ulifanyika mkutano wa kujadili mbinu za kuzuia wizi kwa kutumia mitandao katika nchi za Afrika Mashariki ambapo ilitolewa ripoti kuhusiana na vitendo hivyo.
Akifungua mkutano huo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Silima anabainisha kuwa hapa nchini kuna kesi zaidi ya 300 za uhalifu wa mitandao ambazo zinachunguzwa na baadhi ziko kwenye hatua ya kufikishwa mahakamani.
Katika mkutano huo pia ikabainika kuwa wizi huo umekuwa ukifanyika kirahisi kutokana na nchi za Afrika Mashariki kutokuwa na wataalamu wa kutosha katika kukabili vitendo hivyo haramu.
Wadau wengi wa mitandao kwenye mkutano huo wanaweka wazi kuwa kuna umuhimu wa kubadilishana uzoefu kwa wataalam.
Hii inatokana na ripoti iliyotolewa na Kampuni ya Kaspersky lab ambayo ilibainisha kuwa genge la wahalifu wa mtandao lilifanikiwa kuiba mamilioni ya Dola za Marekani kutoka kwenye akaunti za wateja wa benki 1,000 katika mataifa 30 kati ya mwaka 2014 na 2015.
Wizi huo unaonekana ulianza mwaka 2013 na bado unaendelea kwenye benki mbalimbali, huku kukiwa na mbinu finyu katika kuukabili.
Ripoti hiyo ilitoa mfano wa mbinu za genge la Carbanak, linatumia mbinu ya kuambukiza virusi kwenye mashine na kompyuta za benki ikiwamo kamera za CCTV ili kunakili kila kitu kinachoandikwa kwenye komputa.
Ripoti hiyo inaelezea mbinu mpya za wahalifu mtandao wanazotumia kudukua nambari za akaunti za wateja za siri kabla ya kuingia na kuiba fedha.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, benki katika mataifa 30 yakiwamo, Russia, Marekani, Ujerumani, China, Ukraine na Kanada yameathirika kwa asilimia kubwa.
Kaspersky imesema kuwa wizi huo ulianza mwaka wa 2013 na bado unaendelea hata leo kwani hivyo benki nyingi zinapaswa kuwa makini kwa sababu bado uhalifu huo unaendelea.
Taarifa inaeleza kwamba genge la wahalifu mtandao limefanikiwa kuiba mamilioni ya Dola za Marekani kutoka kwenye akaunti za wateja wa benki 100 katika mataifa 30 kati ya mwaka 2014 na 2015.
Genge hilo la wezi, lililoanzia shughuli zake nchini Urusi, Ukraine na Uchina. Kwa mujibu wa ripoti hiyo benki katika mataifa 30, zikiwamo za Russia, Marekani, Ujerumani, China, Ukraine na Canada.
Uchunguzi mbalimbali wa kimataifa unaonyesha kuwa wezi wamekuwa werevu kiasi kwamba, huweza kutumia teknolojia kupata taarifa za siri za watumiaji wa kompyuta zilizounganishwa kwenye mitandao.
Wanatumia programu mbalimbali zinazoitwa virusi vya kompyuta kupata taarifa hizo. Virusi hao ni kama vile trojans, worms, viruses, hacktools, rootkits na hadware.
“Siku hizi kuna uhusiano wa kampuni hasa kati ya maharamia wa njia za mitandao na kampuni au vikundi vinavyojihusisha na jinai. Hawa ndio wanaojihusisha na jinai na ndio mara nyingi wanakuwa ni chanzo cha kuwezesha kusambaza mafanikio ya wizi kwa njia ya mtandao,” anasema Daniel Kamau kutoka kampuni ya inayojihusisha na utengenezaji wa kompyuta pamoja na programu zake ya Microsoft.
Baadhi ya mitandao inayoibuka na kulaghai kwa kuwataka wananchi, kutoa taarifa zao muhimu za kibenki, jambo ambalo linahatarisha usalama wa fedha zao zinazohifadhiwa na benki hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Dk Charles Kimei anasema kuwa kumeibuka mchezo kwa baadhi ya mitandao ya kijamii, ikijaribu kuwalaghai wateja kwa kuwaomba taarifa za akaunti zao ili kufanya uhalifu.
Alisisitiza wananchi wanatakiwa kuwa makini na kundi hilo, wasikubali kudanganyika kwa kutoa taarifa zinazohusiana na nyaraka nyeti za benki zao na kusisitiza kuwa ni marufuku kutoa taarifa hizo hata kwa wafanyakazi wa benki.
Kauli ya Kimei inawiana na tamko la mitandao ya simu linalowahadharisha wateja wao kutotoa taarifa zao, hasa namba ya siri za akaunti zao za fedha, hata kama wanaozitaka watajitambulisha ni wafanyakazi wa mitandao husika.
Hali hii inaashiria kuwa wahalifu wanatumia teknolojia ili kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu. Hii inaashiria wazi kwamba Tanzania nayo inapaswa kuweka mkakati wa hali ya juu wa kuwa na wataalamu wa kutosha ili kukabiliana na tatizo hilo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment