Image
Image

Tusipotoshe wananchi kwa lengo la kisiasa.

PAMOJA na kampeni za kisiasa za kuwania dola kuanza kwa kishindo nchini, kuna baadhi ya makundi ya watu yamekuwa yakitumia maneno mbalimbali kupotosha ukweli ambao umetamkwa katika moja ya muktadha ya mikutano ya kampeni.
Ingawa kazi ya kila chama cha siasa kilichoundwa nia yake ni kukamata dola na kutekeleza fikira zake, vitendo vinavyofanyika kupotosha maneno na kuyashupalia ni kitendo kinachoonesha udhaifu katika kunadi sera.
Ni vyema kama makundi hayo yakatambua ukweli wa ubaya wa kushupalia na kupotosha ukweli wa mambo kwa manufaa yao binafsi, ili kupata ’kicheko’ kisichostahili kwa hila na ghilba.
Pamoja na upotoshaji mkubwa wa mwenendo wa taifa hili tangu kuanzishwa rasmi kwenye miaka ya sitini, kauli zinazoyumbisha maana halisi ya mambo inatia kichefuchefu na ni vyema wahusika wakaachana na kauli hizo za kupotosha.
Hivi karibuni wakati wa uzinduzi wa kampeni za Chama Cha Mapinduzi, Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa alisema juu ya dhana potofu ya ukombozi inayoshadidiwa na baadhi ya vyama na wagombea wao, huku kiukweli kazi hiyo ya ukombozi ikiwa imeshafanywa na waasisi wa taifa hili Mwalimu Julius Nyerere na Mzee Karume.
Akiwa anatambua kwamba watu wanaofanya kelele hizo, za kudai ukombozi wakati nchi ilishakombolewa, ni watu ambao wanafanya hivyo kwa malengo ya kibinafsi, aliwakumbusha Watanzania kwamba kazi ya ukombozi imefanywa miaka ya 60 na ASP na Tanu wakati huo na kusema kudai kuwa ukombozi haujafanyika ni kauli ya dharau kwa Watanzania na waasisi wa taifa hili.
Na katika kuimarisha usemi wake, alisema wazi kwamba wanaodharau ukombozi uliofanywa na vyama hivyo ni wapumbavu na malofa, tena bila kumtaja mtu alikuwa anasema wazi kuhusu dharau ya kazi iliyofanywa na wazee wa taifa hili.
Haiwezekani kwa watu wenye akili timamu, wanaojua mambo, kusema kwamba taifa hili halijakombolewa na kushawishi vijana ambao sasa ni wengi kudharau historia na kuanzia pale historia inapokoma.
Pamoja na kushupalia kwamba ni kauli ya matusi, ukweli unabaki palepale kwamba hayo si matusi, ni maneno yanayoonesha dhahiri uwapo wa watu ambao wanajua lakini wanakwepa ukweli huo wa kihistoria na hawa lazima wawe wapumbavu ambao tafsiri yake ni mazuzu na majuha tu.
Na hakuna shaka kabisa watu hao ni malofa, si wa fedha, bali wa umasikini wa uelewa na wamekuwa watu kupayapaya. Tunachotaka kusema hapa maneno ya ukweli yasitumike vibaya kwani kwa muktadha wake Rais wa awamu ya tatu alikuwa sahihi kutokana na uchambuzi wa mambo ambao aliufanya.
Tufanye siasa kwa kuzingatia ukweli lakini si kwa kuyumbisha wananchi na kutumia vibaya maneno ambayo yanastahili kutumika kwa wakati huo. Tukumbuke kwamba Rais mstaafu Benjamin Mkapa alikuwa mhariri katika gazeti makini na mahiri na anajua uchaguzi wa maneno na mahali muafaka wa kuyazungumzia na hivyo wananchi wasipotoshwe.
Ni kweli kabisa, katika hili Rais mstaafu hajatukana, bali amewaambia watu wasiokuwa na busara na wanaodharau historia ya nchi waache kuwapotosha wengine kwani wanajua kiundani wanayosema si sahihi.
Ni matumaini yetu kwamba wanasiasa wanaowania kuingia Ikulu hawatasita kuzungumza ajenda zao na kukumbuka historia ya nchi hii ambayo imetufikisha katika mahali pa kuweza kunadi sera za maendeleo na si kudharau historia.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment