Image
Image

Sumatra pangeni Nauli za mabasi ya kasi kwa kuzingatia kipato cha wananchi.

Mamkala ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), juzi ilitangaza kupokea mapendekezo ya nauli kutoka kwa Wakala wa Mabasi ya Mwendo Kasi Dar es Salaam (Dart).

Mapendekezo ya nauli hizo yanatazamiwa kutumiwa na kampuni ambayo itatoa huduma ya usafiri wa umma katika njia na miundombinu ya Dart katika kipindi cha mpito.

Kiwango cha juu kilichopendekezwa na Dart ni Sh. 900 ambacho kitahusu zaidi safari katika njia za pembezoni na njia kuu zilizojengwa kwa ajili ya kutumiwa na mabasi hayo.

Pia viwango vingine vilivyopendekezwa ni Sh. 700 na Sh 500, viwango vinavyotegemea zaidi njia inayotumiwa na wananchi. Kufuatia mapendekezo hayo, Sumatra imetangaza kuwa itakaa na wadau kujadiliana nayo juu ya mapendekezo hayo ya nauli kama yalivyotolewa na Dart.

Hata hivyo, mapendekezo hayo tayari yamezua manung’nuko kutoka kwa wananchi ambao wanaamini kuwa kiasi kilichopendekezwa ni kikubwa kuliko hali halisi ya kiuchumi. Ni dhahiri kwamba usafiri wa mabasi ndiyo tegemeo kubwa kwa wananchi wa kipato cha chini katika Jiji la Dar es Salaam, hivyo kupanga kiasi kikubwa cha nauli kwa vyovyote vile kitawaathiri kwa kiasi kikubwa.

Tunaiomba serikali iangalie suala hili la nauli kwa kuwa tunaamini kwamba uanzishwaji wa mradi wa Dart ulikuwa na nia njema ya kuwapunguzia adha wakazi wa Jiji la Dar es Salaam pamoja na kupunguza foleni.

Mradi wa Dart ulianzishwa kufuatia mkopo wa Dola milioni 290 za Marekani kutoka Benki ya Dunia ambao Serikali ya Tanzania itatakiwa kuulipa. Kwa maneno mengine ni kwamba fedha za umma zitatumika kulipa mkopo wa mradi huo.

Kwa msingi huu, wananchi wengi walikuwa na matumaini kwa kuwa fedha zinazotumika ni za mlipa kodi, kutakuwa na nafuu tofauti na usafiri wa mabasi ya daladala yanayomilikiwa na sekta binafsi. Lakini katika hali ya kushangaza, mapendekezo ya Dart yanatoa picha kuwa mradi huu unaelekea kujiegemeza  katika kutengeneza faida zaidi badala ya kusaidia wananchi wa kipato cha chini waliokuwa wakiisubiri kwa hamu huduma hii. Uzoefu unaonyesha kwa mifano ya nchi mbalimbali duniani kuwa pale serikali inapoweka mkono katika uendeshaji wa usafiri wa umma, nauli zake ni nafuu.

Kitendo cha Dart cha kutaka kutoza nauli za kiasi kikubwa, kitawaumiza wananchi wa kawaida ambao katika wakati huu tayari wana hali ngumu ya maisha ikichangiwa na uduni wa uchumi unaochangiwa kuporomoka kwa thamani ya Shilingi kwa kiasi kikubwa kutoka kwa dola siku za karibuni.

Ni matumaini yetu kuwa Sumatra itasikiliza kilio cha wananchi walio wengi na kuhakikisha kuwa wanapanga bei za usafiri wa mabasi ya Dart zinazoendana na uhalisia wa maisha ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wa kipato cha chini.

Aidha, kwa Dart kupendekeza kiwango hicho cha juu cha nauli, kunaweza kuamsha kilio kutoka kwa wamiliki wa mabasi ya daladala ambao kila mara nao wamekuwa wakililia kupandishwa kwa nauli kwa kisingizio cha kupanda kwa gharama za uendeshaji.

 Tunaomba wadau kujitokeza kwenye mkutano wa kujadili mapendekezo hayo ya nauli za mabasi ya Dart ulioandaliwa na Sumatra ili upatikane muafaka utakaokidhi matakwa ya wananchi wanaolilia usafiri wa uhakika na wa bei nafuu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment