Mhandisi Chambo aliwaagiza watendaji hao kuacha
kufanya kazi kwa mazoea, na badala yake wazingatie Sheria na maadili ya kazi
zao, kutokana na ukweli kwamba sekta ya Nishati ni sekta nyeti inayohitaji watendaji
waadilifu na wabunifu.
“Akitokea mwekezaji ambaye ameonesha nia ni vema
ajibiwe haraka bila kuchelewa iwe amekubaliwa au kukataliwa ombi lake; hakuna
sababu ya kumzungusha mwekezaji; tuzidishe kasi ya uwajibikaji,” alisema
Mhandisi Chambo.
Alisema lengo la Serikali ni kuongeza uwekezaji
hususan kwenye sekta za Nishati na Madini na hivyo hakuna sababu ya kuchelewesha
uwekezaji kwani fursa za uwekezaji zilizopo nchini ni nyingi.
Aliwaasa EWURA na Taasisi nyingine kuacha tabia ya
woga, na kusema kwamba endapo itatokea mwekezaji akatuma maombi ya kuwekeza
nchini, wanapaswa kupitia maombi husika, kujiridhisha na kutoa maamuzi kwa
haraka na kwa kujiamini.
“Tufikie mahali tufanye maamuzi. Msiwe na woga
kwenye kutekeleza jambo lenye maslahi mapana ya Kitaifa; majibu ya njoo kesho
hatutayavumilia,” alisema.
Vilevile Mhandisi Chambo alisema ni vyema taasisi
zilizo chini ya Wizara ya Nishati na Madini zikashirikiana na Wizara katika
kufanya upembuzi yakinifu wa miradi katika maeneo ambayo yanahitaji uwekezaji.
Aidha, aliwaagiza watendaji kukaa pamoja kujadili maeneo ya kipaumbele ili
upembuzi yakinifu ufanyike kwa lengo la kurahisisha majadiliano na wawekezaji.
Alisema ni vyema ikaundwa timu ya wataalamu kutoka
katika Taasisi na Wizara ambao watahusika moja kwa moja na suala la kubaini
maeneo pamoja na kufanya upembuzi yakinifu kwa miradi yenye tija na manufaa na
hivyo kufikia mwafaka mapema na kuanza utekelezaji wa mradi husika pale
mwekezaji anapojitokeza.
“Ikitokea mwekezaji akaonesha dhamira ya kuwekeza
kwenye maeneo husika ni vema taarifa za awali zikawepo. Hii itavutia wawekezaji
wengi zaidi lakini pia itaharakisha majadiliano,” alisema. Aidha, Mhandisi
Chambo aliwapongeza EWURA kwa kufanya vizuri kwenye masuala ya mafuta na
kuwaasa kujitahidi kufanya vizuri katika majukumu mengine yaliyo chini yao.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlagosi aliahidi kufanya kazi kwa
uadilifu na kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na Katibu Mkuu pamoja na kumpatia
ushirikiano wa kutosha.
Kikao hicho ni mwendelezo wa vikao vya Katibu Mkuu
huyo na Menejimenti pamoja na Bodi za Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati
na Madini ili kupata ufumbuzi wa changamoto zinazozikabili.


0 comments:
Post a Comment