Image
Image

Serikali yaipa NDC miezi mitatu kulipa kiasi cha dola za Marekani milioni 2.1.

SERIKALI imelipa Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) miezi mitatu kuhakikisha linapata kiasi cha dola za Marekani milioni 2.1 kwa ajili ya kiwanda cha viuadudu vya kuua viluwiluwi vya mbu wanaoeneza ugonjwa wa malaria, Tanzania Biotech Product Ltd, kilichopo wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Aidha, imesema inashangazwa na shirika hilo kuajiri wafanyakazi 143 Julai mwaka jana kwa ajili ya kiwanda hicho, ambao wanalipwa mishahara ya bure bila kuzalisha kitu chochote.
Hayo yamesemwa mjini Kibaha jana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dk Adelhelm Meru alipotembelea kiwanda hicho ambacho kilizinduliwa Julai 2015.
Dk Meru alitoa agizo hilo kutokana na kutoridhishwa na maombi ya NDC kuomba kiasi hicho serikalini. Maombi hayo yalitoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Shirika hilo, Godwill Wanga, kwa lengo la kufanya majaribio na kuanza uzalishaji.
“Serikali haiwezi kutoa kiasi hicho cha fedha ambazo zingetumika kwa ajili ya huduma za jamii, hivyo fanyeni kila njia ikiwemo kukopa, ombeni hata benki ya uwekezaji nchini (TIB) ili mhakikishe mnapata fedha hizo na majaribio yaanze ili uzalishaji uanze, tumechelewa kwa kipindi cha miaka minne,” alisema Dk Meru.
Alisema inatosha kwani serikali ililipa gharama zote za ujenzi wa kiwanda hicho dola milioni 22 na kilitakiwa kianze kazi tangu mwaka 2012, ikasogezwa hadi Julai 2015. Alisema hadi sasa ni miezi sita imepita, lakini uzalishaji bado.
“Hatuwezi kuwa kioja, tafuteni fedha hizo dola milioni 1 kwa ajili ya majaribio na dola milioni 1.2 kwa ajili ya mtaji, kwani malengo ya serikali ilikuwa kiwanda kianze kazi kwa muda uliopangwa ili kiweze kukabiliana na ugonjwa wa malaria na ziada ya dawa kuuzwa nje ya nchi, hivyo kuweza kufikia malengo yaliyowekwa,” alisema Dk Meru.
“Nataka ifikapo Mei Mosi mwaka huu, mimi nije na Waziri wangu ili tuone uzalishaji unaanza mara moja, kwani moja ya sera za awamu hii ya tano ni kujenga uchumi kupitia viwanda na kuwa nchi yenye uchumi wa kati ili kuleta maendeleo ya wananchi,” alisema Dk Meru.
Awali akielezea juu ya maendeleo ya kiwanda hicho, Wanga alisema kuwa baadhi ya vifaa kwenye mashine viliathiriwa na kukatika kwa umeme, hali iliyosababisha uzalishaji ushindwe kuanza.
Wanga alisema kuwa kutokana na kuchelewa kuanza kazi, ilibidi wataalamu kutoka Cuba, inakotoka teknolojia hiyo ya Labio Farm, kudai gharama zaidi za ujenzi hivyo kudai fidia.
“Kiwanda hiki kinahitaji msaada hata kwa mkopo kiasi cha dola milioni 2.1 ili kuweza kukamilisha hatua zilizobakia kwani wataalamu wetu wameishiwa mtaji baada ya muda kuongezeka na kutokana na matatizo ya kuharibika vifaa vya mashine za kiwanda hiki,” alisema Wanga.
Alisema kuwa teknolojia hiyo ni mpya na uzalishaji utakapoanza, itasaidia kukabiliana na malaria kwani dawa hiyo ina uwezo wa kuua mazalia ya mbu. Alisema baadaye kiwanda hicho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha bidhaa nyingine, ikiwa ni pamoja na mbolea na dawa mbalimbali.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment