Image
Image

Tusizipuuze tahadhari za mvua zitolewazo na mamlaka ya hali ya hewa TMA.

Tahadhari ya kunyesha kwa mvua kubwa katika mikoa kadhaa nchini kuanzia mwezi huu imetolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini  (TMA).
Mamlaka hiyo  imeeleza kuwa zitanyesha mvua katika  maeneo  mbali  mbali  nchini  huku mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Morogoro na Zanzibar ikitarajiwa kuwa na vipindi vifupi vya mvua kubwa kati ya Januari na Februari.
Taarifa ya TMA iliyotolewa jana na Mkurugenzi Mkuu wake, Dk. Agnes Kijazi, ilisema kuwa maeneo  yanayopata misimu  miwili  ya  mvua, Ukanda  wa  Ziwa  Victoria  hususani  maeneo yaliyopo mashariki mwa Ziwa Victoria mikoa ya Mara, Simiyu na Mwanza) na Nyanda za  juu  Kaskazini  Mashariki  yenye mikoa  ya Arusha, Manyara  na  Kilimanjaro yanatarajiwa  kupata vipindi  vya  mvua  katika  miezi hiyo.
Mamlaka hiyo inaeleza kuwa maeneo  yaliyopo  maghariki mwa ziwa Victoria yenye mikoa ya Kagera, Geita na Shinyanga na yale ya kaskazini mwa mkoa wa Kigoma  yanatarajiwa  kupata  mvua ya kawaida.
Taarifa hiyo ilisema yapo maeneo ambayo yatapata mvua kubwa na kuwataka wananchi wanaoishi mabondeni kuchukua tahadhari na kuendelea kufuatilia taarifa rasmi zinazotolewa na Mamlaka hiyo.
Aidha, TMA imesema kuwa hali ya joto inaonyesha kuwa joto limeendelea kuongezeka katika Bahari ya Pasifiki kama kiashiria cha kuimarika kwa El-Niño sambamba na kuongezeka kwa joto katika Bahari ya Hindi kama iliyotarajiwa na kuelezwa katika taarifa ya utabiri wa mvua. 
Kuwapo taarifa kuwa baadhi ya maeneo yatapata mvua kubwa hazinabudi kuwa changamoto kwa mamlaka mbalimbali za serikali na watu binafsi kwa kuwa kuna uwezekano wa kutokea athari mbalimbali. Mvua kubwa zimekuwa zikisababisha mafuriko na nyingine kuambatana na upepo ambao huezua nyumba na kuharibu mazao.
Athari za mafuriko mara nyingi zimekuwa zikiwakumba na kuwaathiri wakazi wanaoishi katika maeneo hatarishi, yakiwamo ya mabondemi na kulazimika kuhitaji misaada ikiwamo ya malazi, chakula, dawa na nyingine za kibinadamu.
Kutokana na athari hizo hususani za mafuriko kuyakumba maeneo ya mabondeni kila mwaka, serikali ya Awamu ya Tano imeshaanzisha operesheni ya kuzibomoa nyumba zote za wananchi waliojenga katika maeneo yasiyoruhusiwa yakiwamo ya mabondeni nchi nzima.
Ingawa kuna baadhi ya watu wanaokaidi agizo la serikali la kuwataka waondoke maeneo hayo, lakini taarifa ya TMA inayotabiri kuwa maeneo kadhaa yatakumbwa na mvua kubwa zinapaswa kupewa umuhimu na kuchukuliwa hatua za tahadhari haraka kuanzia sasa dhidi ya madhara yanayoweza kutokea.
Moja ya hatua hizo ni wananchi waliojenga maeneo hatarishi kukubali kuondoka kwa hiyari yao na kuhamia maeneo mengine, lakini pia na mamlaka za serikali hususan halmashauri kuboresha miundombimu ya barabara, madaraja, mifereji ya maji ili mvua hizo zikinyesha zisilete athari.
Hatua hizo zinapaswa kuchukuliwa kwa kuwa kuwapo kwa taarifa kuwa hali ya joto inaonyesha kuwa joto limeendelea kuongezeka katika Bahari ya Pasifiki kama kiashiria cha kuimarika kwa El-Niño sambamba na kuongezeka kwa joto katika Bahari ya Hindi, ni dalili kuwa mvua za El-Nino zinaweza kuyakumba baadhi ya maeneo nchini na kuleta maafa.
Dalili za kutokea kwa athari katika maeneo ya nchi kuanzia sasa hadi kuanza kwa mvua za masika zimeshaanza kuonekana kwa kuwa tayari kuna maeneo kama ya Mkoa wa Manyara ambayo imenyesha mvua kubwa na kuharibu miundombinu husani barabara na madaraja.

Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment