Image
Image

Uchaguzi wa Kijitoupele utafanyika NEC yasisitiza.

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema kwamba haianzishi na haijaanzisha Jimbo jipya la Uchaguzi baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu, huku ikisisitiza kuwa Jimbo la Kijitoupele mjini Unguja litafanya uchaguzi wake ambao uliahirishwa mwaka jana.
Mkurugenzi wa Uchaguzi, Ramadhani Kailima amesema hayo jana katika taarifa yake kwa umma kuhusu habari iliyoandikwa na gazeti la kila wiki la MwanaHALISI juzi yenye kichwa cha habari “NEC yaibua mapya.”
Kailima alisema hata kabla Tume ya Uchaguzi Zanzibar, haijafuta matokeo wa Zanzibar, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilikuwa imeshatangaza kuahirisha uchaguzi katika majimbo manane, likiwemo la Kijitoupele kwa sababu za vifo vya wagombea na hitilafu mbalimbali.
“Jimbo la Kijitoupele la Zanzibar ni miongoni mwa majimbo nane (8) ambayo yaliahirishwa kufanya uchaguzi wa Wabunge tarehe 25 Oktoba, 2015, ambapo majimbo sita (6) ambayo ni Lushoto, Ulanga Mashariki, Masasi Mjini, Ludewa, Handeni Mjini na Arusha Mjini yaliahirishwa kutokana na vifo vya wagombea na majimbo mawili (2) ya Kijitoupele - Zanzibar na Jimbo la Lulindi – Masasi yaliahirishwa kutokana na hitilafu mbalimbali,” alieleza Kailima.
Kuhusu hoja nyingine iliyotolewa na gazeti hilo kuhusu uteuzi wa wabunge wa Viti Maalumu, Kailima alisema ifahamike kwamba katika maamuzi yake kuhusu Viti Maalumu, Tume imezingatia matakwa ya Ibara ya 78 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Alisema Katiba hiyo inaeleza kuwa ili chama kilichoshiriki Uchaguzi Mkuu, kipate Viti Maalumu ni lazima kiwe kimepata angalau asilimia tano ya kura zote halali za ubunge. “Hivyo, Viti Maalumu vilivyobaki haviwezi kugawanywa hadi hapo Jimbo la Kijitoupele litakapofanya uchaguzi katika tarehe ambayo itatangazwa na Tume hapo baadaye,” alifafanua Kailima.
“Kwa kuwa Mhariri wa Gazeti la MwanaHALISI alikusudia kuupotosha umma kwa sababu anazozifahamu yeye mwenyewe kwa kutoa taarifa zisizo sahihi, za uongo na uchochezi Tume ya Taifa ya Uchaguzi inamtaka Mhariri wa MwanaHALISI kuiomba radhi Tume ya Taifa ya Uchaguzi ukurasa wa mbele wa toleo lijao kama alivyofanya katika toleo hilo. Kama wasipofanya hivyo Tume ya Taifa ya Uchaguzi italichukulia Gazeti la MwanaHALISI hatua za kisheria,” alibainisha Kailima.

Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment