Image
Image

Kufunga kiwanda kwa tatizo la umeme si habari njema sana.

JUHUDI za Serikali ya Awamu ya Tano za kufufua na kujenga viwanda vingi kadri inavyowezekana zimekuwa zikipata changamoto hasa kutokana na umeme kuendelea kutokuwa wa uhakika.
Gazeti hili jana lilibeba habari inayohusu kiwanda cha chuma cha Lodhia Group kinachomiliki kampuni nane hapa nchini kikiwamo kiwanda cha kutengeneza nondo kilichopo mjini Arusha, kupunguza wafanyakazi 340 na kisha kufunga uzalishaji kabisa kutokana na tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara.
Hiyo ni habari mbaya kwa kuwa Serikali hii inayoongozwa na Rais John Magufuli imedhamiria kuinua viwanda na si kuvifunga, na wala kuona wafanyakazi wake wakikosa ajira kwa kuwa lengo la kuweka mikakati ya kufufua viwanda ni moja ya njia ya kuongeza ajira.
Katika habari hiyo, Mkurugenzi wa kampuni ya Lodhia Group, Sailesh Pandit amekaririwa akimwambia Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Luhaga Mpina kuwa umeme umekuwa ni kikwazo kikubwa katika uzalishaji wa nondo kiwandani hapo.
Anasema, kwa saa moja, umeme unaweza kukatika hata mara 10, hivyo kuzorotesha uzalishaji. Hali hiyo imesababisha kiwanda kulazimika kupunguza wafanyakazi na hatimaye kusimamisha uzalishaji kwa kuwa hakuna umeme wa uhakika.
Mkurugenzi huyo akaenda mbali zaidi kwamba, wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu wamekuwa wakifurahia hali hiyo kwa kuwa wanatumia mwanya wa uhaba wa nondo kuingiza nyingine kutoka nje ya nchi ambazo hazikidhi viwango kwa kupitia njia za panya.
Kwa kuwa nia kubwa ya Serikali ni kuongeza viwanda, tunaamini itaweka juhudi zaidi kama alivyosema Naibu Waziri baada ya kusikia kilio cha mkurugenzi huyo katika kuhakikisha Shirika la Umeme nchini (Tanesco) linafanya kila liwezalo kulitafutia ufumbuzi wa kudumu tatizo la umeme katika Jiji hilo la Arusha ambalo ni la kitalii na kibiashara.
Arusha ni Jiji ambalo limekuwa na shughuli nyingi za kitaifa na kimataifa, hivyo kukatikakatika kwa umeme si tu ni adha kwa viwanda, lakini pia ni kikwazo kwa ukuaji wa utalii nchini kwa kuwa jiji hilo ni kitovu cha utalii.
Tunajua serikali inaendelea na mradi uliopewa jina la ‘uti wa mgongo’ kwa kujenga njia ya umeme wenye msongo mkubwa zaidi utakaowezesha kusafirisha umeme mwingi nchi nzima hadi mipakani, Arusha ikiwemo, lakini kabla mradi huo haujakamilika, ni vyema Tanesco ikahakikisha mji kama Arusha inakuwa na umeme wa uhakika ili kuimarisha viwanda, utalii na shughuli zingine za uchumi na kijamii.
Lililotokea katika kiwanda hicho na hasa hatua ya kufunga uzalishaji, linarudisha nyuma juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano katika kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda. Ni katika muktadha huo, tunahimiza watendaji kuwa makini katika kumsaidia Rais kutimiza lengo hili adhimu.
Tunasema hivyo, si kwa kulaumu uongozi mzima wa Mkoa wa Arusha, kwa kuwa wao walikuwa na nafasi ya kutalifutia ufumbuzi suala hilo kabla halijawa kubwa kwa kiasi fulani, nia ni kuwataka watendaji wa Serikali kumsaidia Rais Magufuli katika jitihada zake za kufufua na kujenga viwanda vingi kadri ya uwezo wa nchi.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment