Image
Image

Ngoma inogile, wazee yanga wakimbilia kwa Makonda.

WAZEE wa Klabu ya Yanga juzi walionana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuzungumzia masuala mbalimbali ikiwemo kukodisha timu kwa Mwenyekiti wao Yusuf Manji. Manji aliuomba mkutano mkuu wa dharura wa Yanga akodishiwe timu hiyo kwa miaka kumi na kwamba atakuwa akitoa asilimia 25 ya faida, lakini akipata hasara itakuwa ya kwake. Suala hilo limezua mtafaruku na kuchukuliwa kwa mtazamo tofauti na wanachama wa klabu hiyo waliogawanyika makundi mawili wanaokataa na kukubali mpango huo.
Kikao hicho cha Makonda na Wazee wa Yanga kimekuja siku chache baada ya Manji kutangaza kujiondoa kwenye timu na kujivua uenyekiti kwa kile alichodai kuandamwa kutokana na mpango wake huo hasa baada ya Katibu wa Baraza la Wazee, Ibrahim Akilimali kupinga mpango huo kwenye vyombo vya habari.
Wazee hao wakiongozwa na Akilimali na Hashimu Mhika walitinga kwa Makonda juzi na inaelezwa kuwa na kikao kizito ambacho kilianza saa mbili na nusu asubuhi hadi jioni.
Kikao hicho kimekuja ikiwa ni siku moja baada ya kundi la vijana wa Yanga kuvamia nyumbani kwa Akilimali na kutaka kumpiga kwa kile walichodai kuwa mzee huyo anaivuruga Yanga kwa kauli zake.
Hata hivyo hakuna aliyekuwa ta yari kuzungumzia kikao hicho kati ya Makonda na Wazee ikidaiwa kilichozungumzwa ni siri yao. Akizungumza na gazeti hili jana Makonda alisema: “Ni kweli nilikuwa na kikao na wazee wangu, sipaswi kusema tulijadili nini ila tumeongea mengi, tumeelekezana kwa hiyo yanabaki kuwa siri kati yangu na wazee wangu”.
Kwa upande wa Akilimali akizungumzia jambo hilo alisema: “Yameshaisha hayo, nimeamua kujishusha na kuomba radhi tusameheane, ulimi hauna mfupa, niliteleza, nashukuru tumesameheana na yameisha”.
Inadaiwa Akilimali alimtumia mmoja wa wajumbe wa Bodi ya Wadhamini Francis Kifukwe amuombee radhi kwa Manji ambapo Manji aligoma kumsamehe mpaka pale atakapoomba kupitia vyombo vya habari ambavyo alitumia kumkashifu kwa kumuita mkurupukaji.
“Manji ni jembe langu, namkubali, yaliyotokea ni mgongano tu wa kawaida, tumeshawekana sawa, nimemuomba msamaha kijana wangu, yamekwisha sisi sote tu wamoja,”alisema Akilimali akithibitisha kutakiwa kuomba radhi kwenye vyombo vya habari.
Akizungumzia ombi la Manji kukodisha timu, mjumbe wa Bodi ya Wadhamini Francis Kifukwe alisema: “Mchakato bado, kuna mambo mengi ambayo yanaendelea tulieni, tukiwa tayari kila kitu tutaweka wazi,” alisema.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment