UONGOZI wa Simba umemtaka mfanyabiashara Mohamed Dewji ‘Mo’ kuwapa
miezi sita ili kukamilisha mchakato wa kubadili mfumo wa hisa ndani ya
klabu hiyo.
Uongozi huo wa Simba chini ya Rais wake Evans Aveva na wajumbe wa
kamati ya utendaji wa klabu hiyo walikutana na Mo Dar es Salaam juzi na
kufikia uamuzi huo.
Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alisema jana kuwa kikao hicho ni
muendelezo wa mkutano mkuu wa wanachama wa klabu hiyo wa Julai 31 ambao
waliridhia klabu yao kwenda kwenye mabadiliko ya mfumo wa Kampuni baada
ya Mo kutoa ofa ya kununua hisa 51 kwa Sh bilioni 20.
Hata hivyo tayari wadau mbalimbali akiwemo Mbunge wa Kigoma Mjini,
Kabwe Zitto na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee
na Watoto, Hamis Kigwangalla walitoa maoni yao kwa kutaka mfanyabiashara
huyo kupewa asilimia 40 na asilimia 60 zibaki kwa klabu ambazo zitauzwa
kwa wanachama wengine ili kuepusha klabu hiyo kutawaliwa na mtu mmoja
ambaye atakuwa na sauti na kufanya maamuzi atakayo.
Tayari wanachama wa Simba kutoka matawi mbalimbali wameanza kupewa
elimu ya hisa kuelekea mchakato huo na Jumapili ijayo watanolewa kwa
mara ya pili na mawakala wa soko la hisa pamoja na wanasheria, katika
ukumbi wa TCC Chang’ombe.
Manara alisema kuwa Mo ameahidi kuwapa hisa za bure wanachama wa muda mrefu wa klabu hiyo.
“Mo anataka kuitoa klabu kwenye bajeti ya Sh bilioni 1.2 kwa mwaka
hadi Sh bilioni 5.5 na kwa kuamini mashabiki wa Simba wanahitaji
mafanikio ya haraka, ameahidi kusajili vizuri, kuajiri kocha mzuri,
ambavyo vyote vinaweza kugharimu Sh bilioni 4 na kwamba Sh bilioni 1.5
itakayosalia ataielekeza kwenye mradi wa ujenzi wa uwanja."
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)


0 comments:
Post a Comment