Image
Image

Abiria wawakatae kwa vitendo madereva wazembe

JUMATATU na Jumatano wiki hii zimeweka Watanzania katika hali ya majonzi na taharuki kubwa kutokana na ajali mbili za barabarani, zilizotokea mkoani Njombe Kusini mwa Tanzania na Mwanza katika Kanda ya Ziwa. Katika muda saa zipatazo 48 tu, tulipoteza maisha ya jumla ya Watanzania 25 na wengine zaidi ya 40 wakiachwa majeruhi katika ajali hizo mbili, zilizohusisha mabasi mawili na gari dogo moja.
Ajali ya Jumatatu ilitokea eneo la Lilombwe wilayani Njombe katika mkoa wa Njombe majira ya saa 1.40 usiku, iliyohusisha basi la New Force lililokuwa linasafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Songea mkoani Ruvuma. Sababu ya ajali hiyo, ilielezwa na mashuhuda kuwa ni mwendo kasi.
Nayo ajali ya pili ilitokea jana majira ya saa 12.15 asubuhi, ikihusisha basi la abiria la Super Shem na gari dogo la abiria, zilizogongana katika eneo la Mwamanya wilayani Kwimba katika mkoa wa Mwanza huku basi kubwa likiwa linatoka mkoani Mbeya kwenda jijini Mwanza na basi dogo likitokea kijiji cha Shirima wilayani Kwimba kwenda jijini humo pia.
Sababu iliyotolewa kwa ajali hiyo ya Mwanza ni kwamba dereva wa basi hilo dogo, aliingia barabara kuu bila kuwa mwangalifu na hatimaye kukumbana na basi hilo kubwa na kusababisha maafa hayo.
Upo msemo maarufu usemao ' Ajali haina kinga'. Lakini ni ukweli pia kwamba kama madereva wa mabasi na gari gari hilo dogo, wangefuata sheria na taratibu za usalama barabarani, huenda tusingepoteza maisha ya wenzetu hao na kuwatumbukiza wengine kwenye janga la kujeruhiwa.
Kwa bahati mbaya pia, ajali zote mbili zimetokea wakati tunaadhimisha Wiki ya Usalama Barabarani. Hivi inakuwaje dereva uliyefundishwa ukiwa na akili timamu, unaliingiza gari lako kwenye barabara kuu bila kusimama na kuhakikisha kwamba hakuna gari au chombo kingine; au hata abiria kabla hujaingia moja kwa moja barabara kuu?
Kama ulisomea kweli kazi hiyo na kufuzi vilivyo, unahitaji mafunzo ya ziada gani kuhusu suala hilo muhimu kulifahamu?
Katika ajali ya mkoani Njombe, hali ilikuwa ya kushangaza zaidi. Abiria walionusurika walieleza wazi kwamba kabla ya ajali hiyo kutokea, walinusurika kupinduka mara mbili kutokana na mwendo kasi wa dereva wa basi hilo.
Hivi inakuwaje abiria wote zaidi ya 50, wasichukue hatua ya kumdhibiti dereva husika na msaidizi wake kwa kuwashinikiza wasimamishe basi na kutafuta msaada wa polisi wa usalama barabarani, awanusuru kwa kutafuta ufumbuzi wa hatari inayowakabili?
Tunapenda kutoa mwito maalumu kwa abiria wote, wanaosafiri kwa mabasi ya abiria, kuchukua hatua za makusudi kabla ya kuingia kwenye mabasi hayo, kuhakikisha wanapeana namba ya kuwasiliana na polisi wa usalama barabarani ili wakipatwa na dereva wa aina hiyo, mwenye 'pepo' wa mwendo kasi, aripotiwe polisi.
Lakini pia abiria ambao naamini ni wengi kuliko dereva na wasaidizi wake, wasikubali kuendelea na safari hadi apatikane dereva mwingine, atakayefuata matakwa ya mwendo wa abiria ulio salama. Kinyume chake, tutaendelea kuuawa na madereva wazembe kama hao na kuendelea kutuachia yatima na vilema.
Hali hii sasa tuikatae, kwa abiria kushirikiana kwa vitendo na askari wetu wa usalama barabarani na kuwakataa kwa vitendo madereva wa aina hiyo. Sasa tuseme basi inatosha.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment