Image
Image

Rais Magufuli aagiza Mkandarasi anyang'anywe passport na pia akutana na Wakurugenzi wa AfDB Lindi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, ameagiza kushikiliwa kwa hati za kusafiria za mwakilishi wa kampuni ya ukandarasi ya Overseas Infranstructure Alliance Private Limited ya India Bw. Rajendra Kumar pamoja na wasaidizi wake mpaka hapo kampuni hiyo itakapokamilisha ujenzi wa mradi wa maji wa Ng'apa Mjini Lindi ambao ulipaswa kuwa umekamilika tangu tarehe 17 Machi, 2015.
Mhe. Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo tarehe 03 Machi, 2017 alipotembelea mradi huo ambao unatarajiwa kuzalisha zaidi ya lita za ujazo milioni 5 za maji kwa siku kwa ajili ya wakazi wa Mji wa Lindi ambao wanakabiliwa na tatizo kubwa la maji.
Mhe. Dkt. Magufuli ameelezea kusikitishwa na usimamizi mbaya wa mradi huo ambao tayari kiasi cha Shilingi Bilioni 21.8 zimetolewa kati ya Shilingi Bilioni 29 zilizopangwa kutumika hadi kukamilika kwake, na ameonya kuwa endapo mradi huo hautakamilika katika kipindi cha miezi 4 kuanzia sasa atachukua hatua dhidi ya wanaopaswa kuusimamia.
"Ikipita miezi minne nisilaumiwe, hatuwezi kukubali wananchi wa Lindi wanashida ya maji, fedha zimetolewa, mkandarasi anaamua kupeleka fedha India, mradi umecheleweshwa kwa miaka miwili na mkandarasi hayupo kwenye eneo la ujenzi halafu mnaopaswa kumsimamia mnamuangalia tu wakati sheria zipo, kwa nini hamkumfukuza muda wote huu?" amehoji Mhe. Rais Magufuli.
Mapema akitoa maelezo kuhusu mradi huo Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Gerson Lwenge amesema mradi huo unatekelezwa kwa mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KFW) na Jumuiya ya Ulaya (EU) ambapo hadi sasa umefikia asilimia 85 na kwamba mkandarasi amesimamisha kazi kutokana na kuishiwa fedha.
Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na ameiomba bodi hiyo ishirikiane na Tanzania kutekeleza miradi mikubwa ya uzalishaji wa umeme na ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa "Standard Gauge".
Pamoja na kutoa ombi hilo Mhe. Dkt. Magufuli ameipongeza benki hiyo kwa kutoa mikopo nafuu iliyowezesha kutekelezwa kwa miradi mingi ya maendeleo hapa nchini hususani ujenzi wa barabara lakini ameomba mchakato wa upatikanaji wa mikopo hiyo urahisishwe na kuharakishwa ili miradi mingi zaidi itekelezwe kwa wakati.
"Hapa Tanzania AfDB imefanya mambo makubwa sana, tunaipenda sana benki hii kwa sababu imetuwezesha kujenga barabara nyingi zikiwemo ya Iringa - Dodoma inayounganisha Cape Town Afrika Kusini hadi Misri, barabara ya Namtumbo - Tunduru - Masasi na nyingine nyingi, kwa kweli hawa ni wadau muhimu wa maendeleo" amesema Mhe. Rais Magufuli.
Akizungumza baada ya kikao hicho kiongozi wa Bodi ya Wakurugenzi waliokutana na Mhe. Rais Magufuli katika Ikulu ndogo ya Lindi Bi. Lekhethe Mmakgoshi amempongeza Mhe. Dkt. Magufuli kwa juhudi zake za kuleta mageuzi ya kiuchumi nchini Tanzania na ameahidi kuwaAfDB itaendelea kuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya Tanzania ikiwemo kufanyia kazi  maombi aliyoyatoa kwa Bodi hiyo.
Nae Dkt. Namajeje Weggoro ambaye ni mmoja wa wakurugenzi hao anayewakilisha nchi saba za Afrika ikiwemo Tanzania amesema Tanzania ni nchi inayoongoza kwa kupata mikopo mingi kutoka AfDB na ameongeza kuwa maombi yaliyotolewa na Mhe. Rais Magufuli yatapewa kipaumbele.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Lindi
03 Machi, 2017.

Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment