Image
Image

Mijadala Bunge la Bajeti ilenge kumsaidia mwananchi

Mkutano wa Bunge la 11 la Bajeti unaoanza leo mjini Dodoma, ni muhimu kwa maendeleo ya uchumi wa Taifa letu. Watanzania takriban milioni 50 macho na masikio yao yataanza kufuatilia vikao vya Bunge hivyo kujua mustakabali wao kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Kutokana na umuhimu wake, Bunge hilo hudumu kwa miezi miwili hadi miwili na nusu, matarajio ya Watanzania ni wabunge kutumia muda huo vizuri kuishauri Serikali kutumia fedha za walipa kodi kwa maendeleo endelevu na kuchochea ukuaji wa uchumi kwa mwananchi wa hali ya chini.
Tunafahamu wabunge wameshirikishwa tangu vikao vya kamati na pia wamesafiri maeneo mbalimbali ya nchi kuona maendeleo ya miradi ya Serikali iliyoombewa fedha katika Bunge la Bajeti lililopita, hivyo hatutarajii kusikia wabunge wakiingiza siasa pale hoja inapohusu miradi ya kiuchumi.
Wote tunafahamu uelewa wa wabunge kuhusu masuala ya bajeti ni mkubwa sana, hivyo tunatarajia pamoja na kuchangia kwao kwenye mijadala, pia watatumia lugha nyepesi inayoeleweka kwa urahisi ili kuwawezesha wananchi kufuatilia kwa ukaribu na kuielewa bajeti.
Tunasema hivi kwa maana moja tu, Bajeti ni mkataba kati ya Serikali na wananchi, kwa maana nyingine Serikali inapeleka bungeni maelezo ya namna watakavyotumia kodi za wananchi katika kukuza uchumi na kuwaletea maendeleo.
Hivyo, wabunge ndio wawakilishi wa Watanzania katika kuhoji kwa nia njema ya kinachowasilishwa na Serikali bungeni, kama wabunge hawataweka mkazo kuisimamia Serikali katika matumizi ya fedha, maumivu ya kiuchumi yatarudi kwa wananchi na hata kudhoofisha mapato ya Serikali.
Siyo kazi yetu kuwapangia wabunge hoja za kuzungumza bungeni, lakini wafahamu wananchi waliowapa kura za ubunge, walifanya hivyo kwa matarajio ya kuwa na uwakilishi wenye weledi ndani ya chombo hicho cha kutunga sheria.
Tunaamini na ndivyo ilivyo, hata wabunge wanaotokana na chama tawala hawakuchaguliwa na wananchi ili wakawe wasemaji na watetezi wa Serikali. Pia, tunatarajia hoja za upinzani ziwe za kuboresha na kujenga badala ya kukosoa pekee.
Nia yetu ni kuwashauri wabunge wote kutekeleza jukumu lao la msingi la kuisimamia Serikali kutekeleza ahadi zake walizotoa wakati wakiomba kura kwa wananchi, kuzifanyia kazi kero zao na kwawezesha Watanzania waishi kwa uhuru, amani na utulivu.
Tunachokiona kama siasa zitatawala ndani ya Bunge hili, kuna hatari Serikali ikakosa ushauri wenye kujenga kuhusiana na matumizi ya fedha zinazotokana na kodi za wananchi. Tunawasihi wabunge kutumia nia njema ya Serikali kwa kutoa ushauri wenye kulijenga Taifa.
Ni imani yetu mkutano wa Bunge utakuwa na hoja zenye kujenga zaidi na wabunge watakuwa na ushirikiano katika kuwatetea wananchi ambao ndio walipa kodi. Na wabunge wanalipwa posho na mshahara kutokana na kodi za wananchi.
Watanzania wanatarajia mambo kama vijembe, siasa za matusi na kupotezeana muda kwa kuomba mwongozo wa spika wenye lengo la kuleta malumbano ya kisiasa au kukomoana, havitakuwapo kwenye Bunge hili. Sote tunatarajia litakuwa Bunge la kujenga Tanzania ya viwanda.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment