Image
Image

Nesi atekwa Dar, watekaji wataka Sh5 mil

Watu wasiojulikana wamemteka Muuguzi wa Hospitali ya Mwananyamala, Pili Amiri, huku wakitoa sharti la kupewa Sh5 milioni ili wamuache huru.
Pili, mwenye umri wa miaka 26, alitekwa akiwa nyumbani kwake maeneo ya Mwananyamala Komakoma, saa tano asubuhi, Alhamisi wiki iliyopita na kuingizwa katika gari linalodaiwa kuwa ni la watekaji hao.

Akizungumzia tukio hilo, mjomba wa Pili, Rahim Kangile alisema watekaji hao baada ya kumteka walipiga simu kwa kutumia namba ya Pili wakidai kutumiwa kiasi hicho cha fedha.

“Waliposema wanataka Sh3 milioni, ili wamuache, tuliwatumia lakini hawakufanya hivyo hadi jana, wakasema tuwatumie tena Sh2 milioni, tumetuma leo(jana) lakini mpaka sasa hakuna chochote tulichofanikiwa,” alisema.

Kangile alisema watekaji hao walitoa vitisho kuwa endapo malipo hayo hayatafanyika basi watafanya jambo lolote baya kwa muuguzi huyo.

“Tulipoona wanatoa vitisho tuliwatumia hizo hela lakini hawajafanya chochote la kuonyesha watamuachia Pili,”alisema.

Alisema watekaji hao walitaka fedha zitumwe katika akaunti ya NMB ya Pili, jambo ambalo lilitekelezwa na baadaye ikabainika kuwa miamala kadhaa imefanywa kupitia mtandao wa ATM kutoka kwenye akaunti ya muuguzi huyo.

Akizungumzia iwapo Pili alikuwa na maadui, Kangile alisema hawana chembe ya shaka kama muuguzi huyo alikuwa na ugomvi na watu hadi kufikia hatua ya kumteka.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mwananyamala, Dk Sophiniasis Ngonyani alisema Pili hakutekwa akiwa mazingira ya hospitali, bali akiwa nyumbani kwake na kueleza kuwa wanafamilia wametakiwa kutoa kiasi hicho cha fedha ili aachiwe huru.

“Ni kweli huyu muuguzi wetu ametekwa tangu Alhamisi iliyopita, tumezipata taarifa kutoka kwa ndugu zake, baada ya kutokuonekana nyumbani kwa siku kadhaa,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa mjomba wa wanafamilia, siku moja baada ya watekaji kumteka msichana huyo, walipiga simu wakitaka kupewa kiasi cha Sh3 milioni.

Dk Ngonyani alisema polisi wameshapewa taarifa za tukio hilo na wanaendelea kufanya kazi yao ili kupata taarifa za ndani zaidi.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment