Image
Image

Magufuli fuata nyayo za Mkapa, Kikwete sekta ya michezo.

Baada ya mlolongo mrefu, huku wagombea 38 wakijitokeza kuwania kuteuliwa kuipeperusha bendera ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hatimaye jana Dk. John Pombe Joseph Magufuli aliteuliwa rasmi kuwa mgombea wa nafasi hiyo.

Magufuli aliteuliwa baada ya kuvuka kizingiti cha kwanza na kutinga tano bora akiwa sambamba na Dk. Asha-Rose Mtengeti Migiro, Balozi Amina Salum Ali, Bernard Kamillius Membe na January Yusuf Makamba.

Baada ya mchujo huo nyota ya Magufuli iliendelea kung'ara baada ya kutinga tatu bora na kuwapiku kwa kishindo Dk. Migiro na Balozi Amina, hivyo kuwa mteule wa kuipeperusha bendera ya CCM hapo Oktoba 25, mwaka huu.

Magufuli ambaye alichukua fomu rasmi Juni 5, mwaka huu, ni miongoni mwa baadhi ya wagombea waliochukua fomu kimyakimya tofauti na wagombea wengine maarufu waliochukua kwa mbwembwe kubwa huku wakizindua na kutangaza  nia zao kwa ahadi kibao.

Kuchukua fomu huko kimyakimya huku pia akizunguka kutafuta wadhamini kwa staili hiyo, kunawafanya watu wengi kushindwa kujua kipaumbele chake katika utendaji kazi wake endapo atafanikwa kushinda katika uchaguzi mkuu Oktoba 25.

Awali kwa upande wa soka, wagombea wengi walitoa ahadi ya kuhakikisha Tanzania inapiga hatua na kuepuka kuendelea kugeuzwa 'kichwa cha wendawazimu' kwa kufungwa mara kwa mara na kushindwa kufuzu michuano mikubwa ya kimataifa.

Tunakumbuka vema moja ya ahadi kubwa aliyoitoa na kuitekeleza Rais wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa, wakati wa harakati zake za kuusaka urais kwamba ilikuwa ni kujenga uwanja mpya wa Taifa wa kisasa.

Mkapa alitangaza kipaumbele chake hicho kwa wadau wa michezo na akahakikisha anasimamia mchakato huo na hatimaye kufanikisha zoezi hilo na sasa Tanzania tunajivunia kuwa na uwanja bora kabisa wa michezo huku pia ule wa zamani ukiendelea kukarabatiwa kwa kiwango cha kimataifa.

Pamoja na mambo mengine mengi aliyoyafanya Mkapa, lakini kwa upande wa wadau wa michezo Tambarare Halisi ikiwa namba moja, hatuna budi kumshukuru na kuendelea kumuombea maisha marefu kwa ahadi hiyo iliyotekelezeka.

Rais wa awamu ya nne, Jakaya Mrisho Kikwete, katika mchakato wake wa kusaka urais 2005, kipaumbe chake kwa wanamichezo, aliahidi endapo atafanikiwa kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, serikali yake itahakikisha timu za Taifa, zinapata makocha kutoka nje na itawalipa mishahara katika kipindi chote.
Kikwete alikamilisha mchakato huo kwa Taifa Stars kuanza kunolewa na makocha kutoka Brazil kabla ya baadaye kuwa chini ya Wadenmark na sasa wazawa huku pia ngumi na netiboli zikiletewa makocha kwa nyakati tofauti. 
Kwa hilo pia, wadau wa michezo tutaendelea kumkumbuka Kikwete kwa ahadi yake iliyotekelezeka, hivyo imani yetu  na matarajio ni kusikia anayempokea kijiti, Magufuli nini ambacho atatuahidi wadau wa michezo na kukitekeleza kwa vitendo. 

CCM imemtangaza Magufuli kuwa mgombea wake katika nafasi hiyo ikiwa ni siku nne baada ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) katika viwango vyake vya kila mwezi, kutangaza kuwa Tanzania ni ya 139 baada ya kuporomoka kwa nafasi 12 kutoka mwezi uliopita, nafasi ambayo inaifanya iburuze mkia kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Tambarare Halisi ikiwa mdau namba moja katika sekta ya michezo, linasubiri sasa kusikia Magufuli akivunja ukimya wake na kutangaza endapo atachaguliwa kuwa rais wa Jamhuri ya Tanzania, ataisaidia vipi nchi yetu kuweza kujulikana kimataifa kupitia michezo na hususan mchezo wa soka ambao unaongoza duniani kwa kuwa na mashabiki wengi.

Tunatambua wazi kunahitajika mkakati wa dhati wa kiuwekezaji katika soka la vijana ili kuhakikisha tunaondokana na kuitwa kichwa cha wendawazimu na hilo linahitaji ushirikiano wa pamoja kati ya wadau wa soka, vyama vya soka, klabu na serikali.

Hivyo,Tambarare Halisi tunatarajia kusikia Magufuli naye akitueleza endapo atafanikiwa kuiongoza Tanzania, mbali na ilani ya uchaguzi ya CCM, kipaumbele chake kitakuwa nini katika kuisaidia sekta hii ambayo ni chanzo kikubwa cha mapato na ajira kwa vijana.

Tunatambua ndani ya wiki mbili hizi, vyama vya upinzani navyo vitatangaza wagombea wao katika nafasi hiyo, hivyo wadau wa michezo wanasubiri ili kuweza kupima vipaumbele vyao hatua itakayowafanya wasijutie uamuzi wao wa kura baadaye Oktoba 25, mwaka huu.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment