Image
Image

Niwakati sasa NEC itangaze mipaka ya majimbo wananchi waijue.

Katikati ya mwezi huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ilitangaza majimbo mapya ya uchaguzi 26. Maamuzi ya kutangaza majimbo hayo yanatokana na mamlaka ya Nec chini ya Ibara ya 75 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. Hili ni jukumu la kikatiba na hakuna ubishi kwamba imetimiza wajibu wake.

Ingawa ibara yote ya 75 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaelekeza jinsi majimbo ya uchaguzi yatakavyogawanywa, kifungu kidogo cha (4) ndicho hasa kimezingatiwa kwa kuwa kinasema wazi kuwa Nec inaweza kutekeleza jukumu hilo mara kwa mara angalao kila baada ya miaka kumi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Nec katikati ya mwezi huu majimbo hayo yako katika makundi mawili; mosi, yaliyoanzishwa kwa kigezo cha ongezeko la halmashauri na pili, yaliyoanzishwa kwa kigezo cha ongezeko la idadi ya watu.

Nec ilitaja majimbo ambayo yalianzishwa kwa kigezo cha halmashauri kuwa ni 20 na kuyaorodhesha kuwa ni Handeni Mjini, Nanyamba, Makambako, Butiama, Tarime Mjini, Tunduma, Nsimbo, Kavuu, Geita Mjini, Mafinga Mjini, Kahama Mjini, Ushetu, Nzega Mjini, Kondoa Mjini, Newala Mjini, Mbulu Mjini, Bunda Mjini, Ndanda, Madaba na Mbinga Mjini.

Majimbo yaliyoanzishwa kwa kigezo cha idadi ya watu ni sita na yalitajwa kuwa ni. Mbagala (Dar es Salaam), Kibamba (Dar es Salaam), Vwawa (Mbeya), Manonga (Tabora), Mlimba (Morogoro) na Ulyankulu (Tabora).

Wakati majimbo haya mapya yanatangazwa maeneo mengi nchini yalikuwa yemekwisha kukamilisha kazi ya kuandikisha wapiga kura katika Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa kielektroniki wa kutambua alama za mwili (Biometric Voters Registration –BVR). Kazi hiyo ingali inaendelea katika mkoa wa Dar eas Salaam.

Wakati kazi hii ikiendelea, wananchi wengi wanakabiliwa na changamoto kubwa, kwamba hawajui baada ya kutangazwa majimbo haya mapya wao wanaangukia wapi. Kuna jimbo moja ambalo limegawanywa kuwa mawili, na pengine hata katika kuanzisha halmashauri hizo ipo mipaka mipya imetengwa ili kuhalalisha maeneo ya kiutawala kwa kuanzishwa kwa mamlaka hizo. Mambo haya yote yanafanyika wakati wananchi ambao ni walengwa wengi wakiwa hawajui wanaangukia wapi.

Mathalan, kwa mkoa wa Dar es Salaam majimbo mawili yamegawanywa, haya ni Ubungo na kutoa Ubungo na Kibamba, wakati Temeke na Kigamboni kwa pamoja yamezaa jimbo la Mbagala. Katika mabadiliko hayo, kuna mkanganyiko mkubwa wa mipaka. Wapo wananchi wengi ambao hawajui kwa sasa wanaangukia wapi. 

Tunafikiri ni vema na haki kama Nec itachukua jukumu ya kufafanua kwa kina kwa wananchi kwa njia ya mabango, vipeperushi na matangazo kwenye vyombo vya habari ili kila mwananchi ajijue yuko wapi.

Jambo hili ni muhimu sana hasa inapotiliwa maanani kwamba maeneo mengi ya makazi katika miji yetu hayajapimwa, watu wamejijengea tu holela, kwa maana hiyo ni rahisi watu kujikuta wakivutwa huku na huko kwa maslahi ya kisiasa kama mipaka hii haitakuwa bayana kwa wananchi.

Kwa kuwa kugawa majimbo ni jukumu la kikatiba la Nec, tunaamini kwamba hata kuwaelekeza na kuwaelemisha wananchi juu ya mipaka ya majimbo husika pia litakuwa ni jukumu mojawapo kubwa la Tume ili wananchi wajue fika watawapigia kura kina nani kwa maana ya wabunge na madiwani wakati wa uchaguzi mkuu Oktoba 25, mwaka huu.

Tunajua kwa sasa Nec inakabiliwa na mambo mengi katika kufanikisha mchakato wa uchaguzi mkuu mwaka huu. Pamoja na majukumu hayo, tunaamini elimu kwa raia juu ya mipaka mipya ya majimbo ni jambo la umuhimu pia. Ni kwa kutambua ukweli huo, tunaihamasisha Nec ijipange kuhakikisha kwamba mipaka ya majimbo mapya ya uchaguzi inajulikana vilivyo kwa wananchi wote.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment