Image
Image

Kikosi cha timu ya soka Simba kitaondoka jijini Dar es Salaam Jumatatu.

Kikosi cha timu ya soka Simba kitaondoka jijini Dar es Salaam Jumatatu na kuelekea Zanzibar kuendelea na kambi yake ya kujiandaa na Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara itakayoanza Septemba 12 mwaka huu.

Awali, uongozi wa klabu hiyo yenye makao makuu mtaa wa Msimbazi, Kariakoo ulipanga kuipeleka timu Oman kwa ajili ya kuendelea na mazoezi na pia kucheza mechi nyingine za kirafiki za kimataifa na timu za huko.

Akizungumza na gazeti hili jana, kocha wa Simba, Muingereza, Dylan Kerr, alisema ameikataa kambi ya Oman kwa vile huko kuna hali ya hewa ya joto kali na anaamini akiipeleka timu huko haitawajenga wachezaji wake.

Kerr alisema kwamba kuipeleka timu yake Oman kwa sasa ni sawa na kuumiza wachezaji kutokana na mazoezi waliyofanya awali kabla ya kucheza mechi ya Simba Day ambayo walishinda kwa bao 1-0 lililofungwa na kiungo, Awadh Juma.

"Oman kuna joto sana, kama hatutaenda Zanzibar, napendelea kikosi changu kirejee Lushoto, ni sehemu nzuri ambayo ilisaidia kujenga stamina ya wachezaji na tofauti ilionekana katika michezo iliyocheza, nataka kiwango cha kila mchezaji kiimarike zaidi, najua ligi ni ngumu na ina ushindani," alisema Kerr.

Aliongeza kwamba kipindi kilichobakia anahitaji kuwapa mbinu zaidi wachezaji baada ya stamina kuimarika.

Tangu kuwasili kwa kocha huyo, Simba imecheza mechi saba za kirafiki na imeshinda zote na kati ya hizo, mbili ni za kimataifa.

Simba imepangwa kuanza msimu mpya wa Ligi ya Bara ugenini Mkwakwani, Tanga Septemba 16 mwaka huu dhidi ya African Sports iliyopanda daraja kabla ya kuwavaa Mgambo Shooting kwenye uwanja huo huo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment