Image
Image

Utulivu na amani hii viendelee kutawala.

Kwa kipindi cha zaidi ya miezi miwili nchi ilikuwa katika mchakato muhimu wa kufanya kampeni, uchaguzi na hatimaye kufikia hatua muhimu ya kutangazwa kwa washindi mbalimbali wa ngazi za udiwani, ubunge na Rais wa Jamhuri ya Tanzania.

Baadhi ya wagombea wote walionyesha ukomavu wa kisiasa kwa kukubali na kuridhia matokeo yaliyokuwa yakitangazwa na mamlaka husika, ingawa katika  maeneo mengine kulijitokeza kasoro ndogo ndogo ambazo kimsingi hazikuathiri utulivu na amani kwa kiwango kikubwa.

Ushindi wa zaidi ya asilimia 58 alioupata Dk. John Pombe Magufuli, umepokelewa na wafuasi Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wananchi kwa ujumla kwa nderemo na shangwe zilizotanda katika maeneo  mbalimbali mikoani pamoja na jijini Dar es Salaam.
Umoja wa Waangalizi wa  Ndani wa Uchaguzi Tanzania  (Cemot) pia umepongeza mchakato wa uchaguzi ukisema sheria na kanuni vilizingatiwa na kuheshimiwa.

Waangalizi hao, pamoja na kumpongeza Dk. John Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, walishauri wananchi kuweka kando tofauti zilizojitokeza wakati wa uchaguzi, badala yake waunganishe nguvu kujenga taifa.
Kutokana na makundi mbalimbali kujitokeza kwa wingi kupongeza ushindi wa Dk. Magufuli, wakiwamo wasomi na wananchi wa kawaida waliosema ushindi wa Dk. Magufuli uliotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), umeonyesha hali halisi na mapenzi waliyo nayo Watanzania wengi  kwa mwanasiasa huyo.

Tunaamini kuwa wagombea na vyama vyao walizingatia maelekezo yaliyotolewa na mamlaka inayosimamia uchaguzi, na huo ni uthibitisho wa ukomavu wa demokrasia nchini wa namna walivyoheshimu sheria na kanuni hususani katika ajenda nyeti za nchi.

NEC jana ilikabidhi vyeti kwa wagombea wa nafasi ya u-rais ikiwa ni ishara ya kukamilisha kabla ya hatua ya mwisho ya kuapishwa kwa Rais mpya wa awamu ta tano.

Tunaamini kuwa hatua iliyobaki ya kumwapisha Dk. Magufuli kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa awamu ya tano inasubiriwa kwa hamu na kupewa ushirikiano ili aweze kutimiza malengo yake kwa Watanzania ya kuondoa kero mbalimbali zinazoikabili taifa.

Ni imani yetu kuwa serikali atakayoiunda Dk. Magufuli itazingatia yote yaliyotangazwa katika Ilani ya uchaguzi ya  CCM ambayo kimsingi ndiyo dira iliyokiwezesha chama hicho kupata ushindi huo na ni wakati wa kuanza kutekeleza ahadi zilizotolewa wakati wa kampeni ili kuleta tija kwa maendeleo ya nchi na wananchi wote bila kujali itikadi zao za vyama.

Tunaamini pia kuwa CCM kitasimamia mambo muhimu ili dhana nzima ya mabadiliko ipatikane kwa wakati kama Dk. Magufuli mwenyewe alivyowaahidi wananchi wakati wa kampeni zake.

Wananchi wanahitaji kupata mabadiliko ya kweli, yatakayogusa nyanja mbalimbali za maisha yao ikiwemo masuala ya kiuchumi, kijamii, kielimu  na uboreshaji wa miundombinu kwa maslahi ya wakulima , wafanyakazi na wafanyabiashara.

Ni imani yetu kuwa kila mwananchi sasa atajiimarisha katika uzalishaji wa bidhaa za kujenga uchumi binafsi na utakaolinufaisha taifa katika eneo lake. Mabadiliko ya kweli yanakuja kwa kufanyakazi kwa bidii.
Ni matumaini ya wengi kuwa tofauti zilizojitokeza wakati wa kutafuta ushindi sasa zitawekwa kando na kuungana ili kulijenga taifa kwa pamoja na kuleta mabadiliko ya kweli.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment