Image
Image

ZEC itabeba lawama Zanzibar ikichafuka.

Dunia imeshtushwa na uamuzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kufuta uchaguzi mkuu wa rais na wawakilishi visiwani huko kwa kile alichosema Mwenyekiti wake, Salim Jecha, kukabiliwa na vikwazo vingi ambao unaufanya usiwe huru na wa haki.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari aliyoisoma mbele ya waandishi, Jecha alitoa sababu tisa alizosema ni kasoro zinazofanya uchaguzi huo kuwa batili.

Baadhi ya sababu hizo ni pamoja na idadi ya kura kuzidi wapigakura walioandikishwa katika baadhi ya vituo; uhamishwaji wa masanduku ya kura kinyume cha taratibu na kura kuhesabiwa kwingineko; kuvamiwa kwa vituo vya kura na vijana walioandaliwa; vyama kujitwalia majukumu ya tume na makamishna wawili wa tume kupigana.

Sababu hizo na nyingine ambazo hakuzifafanua, ndizo alizieleza kuwa msingi mkuu wa kufutwa kwa uchaguzi huo na kwa maana hiyo utafanyika mwingine.

Uamuzi huo umeibua kauli mbalimbali kutoka kwa wadau wa uchaguzi huo. Wa kwanza kabisa kueleza mshituko wake na kuukataa uamuzi huo ni mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad.

Jumuiya ya kimataifa kupitia waangalizi wake, kama Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Madola na Umoja wa Ulaya (EU), kwa pamoja wametoa tamko la kuzitaka serikali za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuingilia kati ili haki za wananchi katika kuchagua viongozi wake ziheshimiwe kwa kuhakikisha kwamba mchakato wa uchaguzi       mkuu wa 2015 Zanzibar unafika mwisho mwema.

Mbali na waangalizi hao, ubalozi wa Marekani nao umeungana na waangalizi wengine wa nje wa kimataifa kueleza kushtushwa kwao na uamuzi wa ZEC kufuta uchaguzi huo.

Ni jambo la bahati mbaya uamuzi wa kufuta uchaguzi wa Zanzibar unatonesha kwa kiwango cha juu kabisa makovu ya vidonda vya zamani juu ya uhasama ndani ya jamii ya Wazanzibari ambao ulipandikizwa tangu zama za utawala wa Mwarabu. Ni uhasama ambao mapinduzi ya Januari 12, 1964 yalilenga kuuondoa ili kujenga jamii mpya ya watu wanaoheshimiana na kujali utu wa mtu.

Ni jambo la bahati mbaya kwamba uhasama huu ambao ulifumuka kwa kasi kubwa baada ya mvurugano wa uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 na kisha kuendelea kuitesa jamii ya Wazanzibari baada ya uchaguzi wa mwaka 2000, lakini tiba ikaanza kupatikana baada ya uchaguzi wa mwaka 2010, sasa unaibuliwa upya tena kwa kishindo.

Tunasikitika, kwamba ZEC imeibuka na uamuzi huu katika kipindi ambacho Watanzania kwa umoja wao na hata jamii ya kimataifa ilikuwa inatazama Zanzibar kama mfano mmojawapo wa jamii iliofanikiwa kusuluhisha matatizo yake na kujenga mustakabali mpya wa maisha yao.

Hakika ni fedheha kwamba ZEC imeibuka na uamuzi wa kufuta uchaguzi huku ikitoa sababu nyepesi mno ambazo zinaacha maswali mengi yasio na majibu. Kwa mfano, katika sababu zote ambazo zimetajwa hakuna hata moja iliripotiwa ama na vyombo vya habari au waangalizi wa uchaguzi siku ya kupiga kura.

Kila tunapotafakari uamuzi huu tunajawa na hofu kwamba Zanzibar itaingia katika machafuko, na kwa hakika wa kubeba lawama atakuwa ni ZEC.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment