Image
Image

Ufisadi mwingine wa Makontena 11,884 na magari 2,019 yabainika kutolewa Bandari ya DSM bila kulipiwa ushuru.

MAKONTENA mengine 11,884 na magari 2,019, yamebainika kuwa yametoroshwa katika bandari kavu (ICD) saba jijini Dar es Salaam bila kulipiwa ushuru wa bandari, hivyo kuipotezea Serikali mapato ya Sh bilioni 48.55.
Kutokana na hatua hiyo, Serikali imeamuru wafanyakazi 15 waliokuwa wanahusika na ukusanyaji wa tozo kutoka katika bandari kavu hizo, wachukuliwe hatua za kinidhamu. Kati ya hao, watumishi saba wameshakamatwa na Polisi wakati wafanyakazi wengine wanane, wametoroka na wanatafutwa na Polisi.
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari(TPA), pia imetoa orodha ya mawakala wa forodha 280, ambao wanatuhumiwa kuhusika na kutolewa kwa makontena na magari bila kulipa tozo za bandari.
Wametakiwa walipe fedha hizo ndani ya siku saba na wasipofanya hivyo watakamatwa, kuchukuliwa hatua na wakishindwa kufanya hivyo watapigwa marufuku kufanya biashara na TPA.
Upotevu ulivyobainika Upotevu wa makontena hayo, ulijulikana baada ya TPA kufanya uchunguzi wa kina katika bandari kavu saba, kubaini kama kuna upotevu mwingine wa mapato ya bandari mara baada ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kubaini awali upotevu wa makontena 2,400, ambayo hayakulipiwa ushuru wa bandari.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, alisema jana kuwa kutokana na ukaguzi huo, imebaini kuwa makontena hayo 11,884 na magari 2,019 yalitolewa bandarini bila malipo kuanzia Julai 2014 hadi Aprili 2015.
Upotevu huo kwa mujibu wa Profesa Mbarawa ulifanywa katika ICD za MOFED ambako makontena 61 yaliyostahili kulipiwa tozo ya bandari ya Sh Sh milioni 513.7 yalipotea, kwenye bandari kavu ya DICD makontena 491 yenye thamani ya Sh bilioni 3.9 yalipotea na EFAG ambako makontena 1,450 yenye thamani ya tozo ya Sh bilioni 7.9 yalipotea.
Alisema makontena mengine yalipotelea kwenye ICD ya AZAM ambako kulikuwa na makontena 295 ya tozo ya Sh bilioni 1.5 na PMM makontena 779 ya thamani ya Sh bilioni 4.4.
Pia AMI makontena 4,384 ya tozo ya Sh bilioni 14.4 na bandari kavu ya TRH ilikuwa na makontena 4,424 ambayo yalikuwa yalipiwe ushuru wa Sh bilioni 14.6 lakini yakaondolewa bila kulipiwa tozo ya bandari.
Kwa upande wa magari, Profesa Mbarawa alisema katika bandari kavu (ICD) ya TALL kulikuwa na magari 309 ambayo yalikuwa yalipiwe tozo ya Sh milioni 242.5, ICD ya CHICASA magari 65 ya thamani ya tozo ya Sh milioni 16.4, FARION magari 18 ya tozo ya Sh 46.4, SILVER magari 97 ya tozo ya Sh milioni 168.9, MASS magari 171 ya tozo ya milioni Sh 32.8 na HESU ambako magari 1,359 yaliyokuwa yalipiwe tozo ya Sh bilioni 1.1 lakini yaliondolewa bandarini bila kulipiwa tozo hiyo ya bandari.
Saba washikiliwa, nane watoroka Kutokana na upotevu huo, Profesa Mbarawa alisema Polisi inawashikilia watumishi saba ambao walikuwa wanahusika na kutoza tozo hizo kutoka katika bandari hizo kavu. Wafanyakazi hao ni John Elisante, Leticia Masaro, Christina Temu, Merina Chawala, Adnan Ally, Masoud Seleman na Bendadeta Sangawe.
Watumishi wanaotuhumiwa kuwa wametoroka na wanatafutwa na Polisi ni Aron Lusingu, Amani Kazumari, John Mushi, Valentine Sangawe, Happygod Naftai, Bonasweet Kimaina, Zainab Bwijo na Nathan Edward.
Mawakala 280 kitanzini Profesa Mbarawa alisema Serikali imeshatoa orodha ya majina 280 ya mawakala wa forodha kwenye magazeti mbalimbali, likiwemo gazeti hili, ili wawasilishe vielelezo vya malipo waliyofanya katika bandari hiyo.
Alisema mawakala ambao watabainika kuhusika kufanya wizi huo, wanapewa muda wa siku saba wawe wameshalipa na watakaoshindwa kulipa baada ya muda huo, watakamatwa na kufikishwa Polisi, ili walipe na kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kufungiwa kufanya biashara na bandari.
Waziri huyo alisisitiza kuwa Serikali haitamvumilia mfanyakazi yeyote wa TPA, awe mkubwa au mdogo, ambaye ataendelea kujihusisha na upotevu wa mapato ya bandari.
“Mawakala wote wa forodha ambao wataendelea kushirikiana na wafanyakazi wa bandari kutoa mizigo bila kulipia tozo ya bandari, Serikali itawafutia leseni za kufanya biashara,” alisema Profesa Mbarawa.
TPA yakusanya Sh milioni 900 Kuhusu makontena 2,431, ambayo wahusika walipewa siku saba na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wawe wamelipia ushuru wa bandari tayari Sh milioni 900.7 kati ya Sh bilioni 1.9, zimeshakusanywa baada ya mawakala 22 kulipa kwa hiyari na wengine kwa lazima.
Akifafanua malipo hayo, Profesa Mbarawa alisema ndani ya siku saba za notisi, mawakala saba waliweza kulipa Sh milioni 80.2. Alisema baada ya muda waliopewa mawakala ambao walikuwa hawajalipa, TPA ilisitisha kufanya nao biashara hadi walipe na baadhi yao walianza kukamatwa na Polisi.
Alisema hadi juzi, mawakala 15 walikuwa wamekamatwa na wote walilipa kiasi walichokuwa wanadaiwa ambacho ni Sh milioni 820.5. “Kutokana na hatua hizo Sh milioni 900.7 zimelipwa hadi kufikia jana (juzi),” alisema.
Alisema ukamataji unaendelea dhidi ya mawakala, ambao hawajalipa fedha wanazodaiwa na lengo ni hadi ifikapo Januari 10 mwaka ujao wote wawe wamekamatwa na kufikishwa Polisi ili walipe fedha zote wanazodaiwa.
Wazungumzia malalamiko ya TAFFA Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Edwin Ngonyani alisema Serikali tayari imepokea malalamiko kutoka kwa Chama cha Mawakala (TAFFA) kuhusu baadhi ya wanachama wao, ambao wanadaiwa kulipa ushuru huo lakini wanadaiwa na TPA.
“TAFFA ni taasisi na wameshaleta barua yao ya malalamiko wizarani, tumewaomba watuorodheshee wanachama wao wanaolalamika na aina ya malalamiko kwa kila mwanachama,” alisema Ngonyani.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Alois Matei alisema mamlaka yake imeanza kuyafanyia uchunguzi madai ya TAFFA kuwa kuna maofisa wa bandari, ambao wanashirikiana na benki mbalimbali kuhujumu mapato ya bandari hiyo.
“Ni kweli tumeanza uchunguzi maana kuna baadhi ya mawakala wameleta vielelezo kuonesha walilipia makontena yao, lakini tulipokwenda benki tulikuta hundi aliyolipia inaonesha malipo yalienda kulipia mizigo mingine,” alisema Matei.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment