Image
Image

Sakata la Kitwanga laibua Mapya*NDUGAI afichua wabunge wavutao bangi na unga.

KAMA unashangaa kusikia kwamba aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, ametimuliwa kwa kuingia bungeni akiwa amelewa.
Bila shaka utachoka zaidi ukisikia kuna wabunge kadhaa huingia kwenye ukumbi wa Bunge wakiwa wametumia vilevi vikali zaidi vikiwamo bangi, viroba na dawa za kulevya.
Spika wa Bunge, Job Ndugai, ndiye aliyefichua siri hiyo jana wakati akizungumza na Nipashe juu ya hatua ya Rais John Magufuli kumtimua Kitwanga katika Baraza lake la Mawaziri kwa sababu aliingia bungeni na kujibu swali la wizara yake akiwa amelewa.
Kutokana na hali hiyo, Ndugai alisema sasa wanafikiria kuweka vifaa maalumu vya kupima ulevi kwa watunga sheria hao na kutafuta wataalamu wa ushauri nasaha watakaowapa msaada wa kisaikolojia.
“Kikubwa tunataka kuweka mkakati wa kujaribu kumtambua (mbunge) mmoja mmoja na kujaribu kuwatafuta wale watu wanaotoa ushauri nasaha au watu wa mambo ya saikolojia.
“Tunajaribu ku-identify (kuwatambua) watu maalum wanaoweza kutusaidia kuzungumza na hawa watu ili waondokane na matatizo yale ambayo tutaweza kuyagundua… lakini wale wanaofanya kwa kificho itakuwa tabu kidogo. Lakini huko mbele tutakwenda kwenye vifaa,” alisema Ndugai na kuongeza:
“Maana siyo ulevi tu, kuna sigara kubwa (bangi), unga (dawa za kulevya)… watu wanapiga konyagi hadi mchana, kimsingi mambo ni mengi,” alisema Ndugai.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa kwa taarifa hiyo asieleweke vibaya kuwa ni wabunge wote hutumia vilevi kabla ya kuingia bungeni, bali wapo wachache wenye kawaida hiyo na kwamba hao ndiyo wanaostahili kusaidiwa na wataalamu wa saikolojia na pia kufunga vifaa maalum vya kuwabaini.
“Simaanishi wote (wabunge), maana mtu anaweza kufikiri ni wabunge wote… hapana. Hili ni kundi dogo mno la wabunge (na) hawajai hata mkononi. Lakini wabunge walio wengi ndiyo wazuri sana, hawanywi pombe wala nini. Kikundi hiki kinahitaji msaada wa ushauri,” alisema.
KUBADILI KANUNI
Akiendelea kufafanua, Ndugai alisema: “Tatizo ni kubwa kiasi… na siyo la kulewa peke yake, lazima kuangalia namna gani ya kumbana mtu yeyote ambaye amelewa, (kama) ametumia madawa ya kulevya.

“Kwa hiyo linatakiwa suala la kubadili kanuni litazamwe kwa mapana, siyo leo unadhibiti aliyelewa, kesho unadhibiti hali hii… ni lazima kuliangalia (suala hili) kwa mapana yake,” alisema Ndugai.
Alisema tofauti na kikao cha asubuhi ambacho ndicho Kitwanga aliingia akiwa amelewa (Ijumaa Mei 20, 2016), kile cha jioni ndiyo huwa kibaya zaidi.
“Nakubaliana ipo haja ya kuwa na vifaa, hasa bunge la mchana ndiyo huwa (na tatizo) zaidi, maana kuna baadhi ya wabunge wanakuja pale mchana wameshalewa,” alisema.
Alisema wabunge hao ambao huingia bungeni wakiwa wameutwika, kubwia unga ama bangi, wakati mwingine hutibua vikao vya Bunge.
“Huyo mbunge mmoja au wawili, wanaweza kutibua Bunge …ukajikuta Bunge zima linatibuka kumbe wenzenu hawapo `normal’ (kawaida). Kwa hiyo tunaendelea kuangalia (namna ya kudhibiti hali hiyo) kwa kupewa mawazo na Watanzania,” alisema Ndugai.
Alisema wakati mwingine Kamati ya Bunge ya Maadili inakaa na kufanya maazimio juu ya mbunge fulani, kumbe ukweli ni kwamba mhusika hakuwa sawa wakati akifanya tukio hilo la kukiuka kanuni bali anakabiliwa na msukumo ‘fulani’.
HATUA DHIDI YA KITWANGA
Akieleza kuhusu hatua watakazozichukua dhidi ya Kitwanga ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Misungwi, Ndugai alisema hawafikirii kumpa adhabu yoyote baada ya ile ya kuondolewa uwaziri.

“Kuhusu Kitwanga, hatuwezi kumchukulia hatua yoyote ile. Kama ni mlevi sana, anatakiwa kufanyiwa `counseling’ (kupewa ushauri nasaha) ili kuondokana na hilo tatizo. Mimi siwezi kujiunga na wale ambao wanamsakama, mimi ni baba na mama wa wabunge wote… kwa yule ambaye ameteleza, mimi ni wajibu wangu kumrudisha kwenye mstari. Ndiyo kazi nitakayofanya.”
Siku ya Ijumaa (Mei 20), majira ya jioni, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa, alitoa taarifa kwa vyombo vya habari juu ya hatua ya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa Kitwanga kwa sababu ya kuingia bungeni akiwa amelewa.
“Rais Magufuli ametengua uteuzi huo kufuatia kitendo cha Mheshimiwa Charles Kitwanga kuingia bungeni na kujibu swali linalohusu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi akiwa amelewa.”
Akizungumzia uamuzi wa Rais kumuondoa Kitwanga, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alisema uamuzi huo ulikuwa sahihi na swali ambalo Kitwanga hakulijibu vizuri kutokana na hali ya ulevi aliokuwa nao bungeni litajibiwa upya na serikali baada ya wabunge kuomba mwongozo wa swali hilo.
Alisema uamuzi wa Rais Magufuli umefuata kanuni za utumishi wa umma ambazo zinakataza mtumishi kulewa akiwa kazini.
Ingawa Majaliwa hakutaja kanuni hiyo, Kifungu cha 34 cha Sheria ya Utumishi wa Umma ya Mwaka 2002 pamoja na Kanuni ya 65 (1) ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003, kinasema, “Watumishi wa Umma wanapaswa kuepuka tabia ambayo inavunja heshima ya utumishi wao kwa umma hata wanapokuwa nje ya mahali pa kazi.
Tabia inayoweza kuvunja heshima hiyo inatajwa kuwa ni pamoja na matumizi ya dawa za kulevya, ulevi, kukopa kwa kiwango ambacho hawawezi kurejesha na pia kujihusisha na vitendo vyovyote viovu mbele ya jamii.
Hivi karibuni, kabla Rais Magufuli kutengua nafasi yake, Kitwanga alikuwa akishinikizwa na wabunge, hasa wa upinzani kuwa ajiuzulu baada ya kuhusishwa na na Kampuni ya Infosys ambayo inadaiwa kutoa ushauri kwa Kampuni ya Lugumi Enterprises iliyopewa zabuni yenye utata ya kufunga vifaa vya kuchukulia alama za vidole (AFIS) katika vituo vya polisi nchini.
Inadaiwa kuwa kampuni ya Lugumi ililipwa sh. bilioni 34 na Jeshi la Polisi ili kufunga vifaa hivyo nchi nzima katika vituo 138 vya polisi lakini ni vituo 14 tu ndivyo vilivyofungiwa vifaa hivyo, ingawa tayari ilishalipwa fedha hizo (Sh. bilioni 34) ambazo ni sawa na zaidi ya asilimia 90 ya malipo yote ya kazi hiyo.
Share on Google Plus

Kuhusu TAMBARARE HALISI

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment